Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - HABARI ZA LEO - Tanzania yataka watangazaji wa Kiswahili UN waongezwe

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter

TANZANIA imeitaka Idara ya Habari na Mawasilliano ya Umma  ya Umoja wa Mataifa (UN) kuhakikisha kuwa inaongeza idadi ya waandishi katika Idhaa ya Radio ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa ili iweze kutekeleza kwa ukamilifu majukumu yake ya ukusanyaji, utoaji na  usambazaji wa taarifa zinazohusu  shughuli za umoja huo.

Taarifa iliyotolewa jana na Ubalozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa ilieleza kuwa Tanzania imetoa wito huo wakati wa mkutano wa 33 wa Kamati ya Habari ya Umoja wa Mataifa.

Pamoja na mambo mengine kamati hiyo iliyoanzishwa mwaka 1978 ikiwa na wajumbe 113 kutoka nchi wanachama  wa Umoja wa Mataifa, juzi hiyo walipokea na kujadili taarifa ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, kuhusu utendaji wa idara hiyo.

Akizungumza kwa niaba ya  Balozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Ofisa Ubalozi Mwandamizi, Maura  Mwingira alisema katika mkutano huo, Tanzania inafarijika na kuridhishwa na namna ambavyo lugha ya Kiswahili kupitia Radio ya Kiswahili ya UN imeendelea kuwa kiungo muhimu cha mawasiliano, kupata umaarufu na kuongeza idadi ya watumiaji wa taarifa za idhaa hiyo licha ya kwamba ina wafanyakazi wachache.

Taarifa ya Katibu Mkuu wa UN iliyowasilishwa kwa wajumbe na Katibu Mkuu Msaidizi anayeongoza Idara ya Habari, Akito Akasaka, imeonyesha kuwa, katika eneo la Radio ya Umoja wa Mataifa, Radio hiyo ambayo hutoa taarifa zake katika lugha sita rasmi za UN, na lugha mbili za Kiswahili na Kireno, imekuwa na mafanikio makubwa ambayo pia yamehusisha ongezeko la watumiaji wa taarifa zake.

Lugha rasmi za Umoja wa Mataifa ni Kiingereza, Kifaransa, Kiaarabu, Kirusi, Kichina na Kihispania, Kwa upande wa Idhaa ya Kiswahili, Akasaka alisema, Radio hiyo ambayo ilianzishwa mwaka 2006, idadi ya watumiaji wa taarifa za idhaa hiyo imepanda kutoka asilimia moja wakati wa kuanzishwa kwake hadi kufikia asilimia 21, ikiwa ni pamoja na kuanzishwa kwa Radio  Maarifa FM iliyoko Tanzania.

“Haya si mafaniko madogo, ni mafanikio  makubwa ambayo  kila mmoja wetu anapashwa kujivunia na tunawapongeza wafanyakazi hao wawili kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya”, alisisitiza ofisa ubalozi.

Idhaa hiyo ina wafanyakazi wawili tu,  inaongozwa na Mtanzania, Flora Nducha.Ni kutokana na uchache huo wa wafanyakazi, ndio maana Tanzania imeitaka sekretarieti ya Idara hiyo ya Habari ya Umoja wa Mataifa kuangalia uwezekano wa kuongeza wafanyakazi.  Idhaa nyingine  zina wafanyakazi zaidi ya wanne.

Tanzania imewaeleza wajumbe wa Mkutano huo  kuwa Lugha ya Kiswahili ambayo inazungumzwa na zaidi ya watu milioni 200 katika eneo la Afrika ya Mashariki, Afrika ya Kati na nje ya maeneo hayo kwamba ni kiungo muhimu  cha upashanaji wa habari hususani katika udhibiti wa migogoro na ujenzi wa amani.

 Ni kutokana na  umuhimu wa lugha hiyo, Tanzania imesema, ndio maana Umoja wa Afrika uliamua kwa makusudi kabisa kuifanya lugha ya Kiswahili kuwa  kati ya lugha rasmi za umoja huo. “Kiswahili ni lugha muhimu sana kama chombo cha mawasiliano katika Umoja wa Mataifa na katika suala zima la  ulinzi, usalama na ujenzi wa amani na maendeleo.

Tunatambua changamoto ya ufinyu wa bajeti  inayoikabili   Idara ya Habari na Umoja wa Mataifa kwa ujumla wake,  Lakini bado tunaamini kwamba  mtafikiria suala la kuongeza idadi ya wafanyakazi katika idhaa hiyo hivi karibuni,” akasisitiza  Ofisa Ubalozi Mwandamizi.

0 comments

Post a Comment