Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - HABARI ZA KITAIFA , HABARI ZA LEO - Mishahara yapanda

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bi. Hawa Ghasia (katikati) akiwa na wafanyakazi wa wizara hiyo
SERIKALI imetangaza kurekebisha mishahara ya watumishi wake kwa asilimia 40.2 kwa kuzingatia uwezo wake wa bajeti, makubaliano yaliyofikiwa na
Baraza la Majadiliano ya Pamoja na kukabiliana na kasi ya mfumuko wa bei.


Kutokana na hatua hiyo, fungu la mishahara limeongezwa kwa sh bilioni 938, sawa na ongezeko la asimilia 40.2 ya fedha zilizotengwa kugharamia mishahara mwaka jana.


“Kiasi hiki cha fedha kwa ajili ya kulipa mishahara kimeongezeka kwa sh. bilioni 938 ambayo ni sawa na ongezeko la asimilia 40.2 ya fedha zilizotengwa kugharamia malipo ya malipo hayo kwa mwaka wa fedha 2010/2011,” alisema Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bi. Hawa Ghasia wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya ofisi yake ya mwaka 2011/2012.


Katika mwaka wa fedha 2011/2012 serikali inatarajia kutumia sh. trilioni 3.2 kwa ajili ya malipo ya mishahara, upandishwaji vyeo na kulipa madai ya malimbikizo mapunjo ya mishahara kwa watumishi wa Serikali Kuu, Serikali za Mitaa, Wakala na Taasisi za Serikali.


Mbali na hayo, alisema kuwa katika mwaka huu wa fedha, serikali inatarajia kuajiri watumishi wapya 64,024 ambapo kipaumbele kitakuwa katika sekta ya elimu, afya, kilimo na mifugo huku ikitarajia kuwapandisha vyeo wengine 80,050 kwa kada mbalimbali.


Alisema kuwa katika jitihada za kuboresha maslahi ya watumishi wa umma, serikali itaendelea na utekelezaji wa sera ya malipo ya mishahara na motisha katika utumishi wa umma ya mwaka 2010.


Aidha alisema kuwa wizara yake itashirikiana na Wizara ya Fedha katika siku maalumu ya kulipa mishahara ya watumishi wa umma katika vituo mbalimbali vya malipo badala ya mishahara kupitia benki kwa lengo la kuondoa tatizo la watumishi hewa.


Kutokana na majukumu na mipango ya utekelezaji kwa mwaka 2011/2012, aliwasilisha mapendekezo ya maombi ya fedha, ambapo katika fungu 20, Ofisi ya Rais Ikulu, iliombewa sh. bilioni 8.5, fungu 30, Ofisi ya Rais na Sekretarieti ya Baraza la
Mawaziri iliombewa sh. bilioni 200.5 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na sh. bilioni 66.7 kwa ajili ya maendeleo.


Fedha zingine zilizoombwa ni pamoja na fungu 32, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, sh. bilioni 16 ya matumizi ya kawaida, miradi ya maendeleo sh. bilioni 17.3, fungu 33, Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi sh. bilioni 2.3, miradi sh. milioni 910, fungu 67, Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Ajira katika utumishi wa umma sh. bilioni 2.9 na fungu 94, Ofisi ya Rais, Tume ya Utumishi wa Umma, sh. bilioni 8.2 kwa ajili ya matumizi ya kawaida.


Kwa upande wa kambi ya upinzani, walipendekeza kiwango cha mishahara cha kima cha chini kutoka sh. 135,000 ya sasa hadi 315,000 ili watumishi wakabiliane na makali ya kupanda kwa gharama za maisha.


Aidha kambi hiyo, ilipingana na fumula inayotumika sasa katika kuongeza mishahara ya watumishi kwa kufuata kiwango cha asilimia, ikisema ni cha kibaguzi na upendeleo kwa kuwa hupendelea zaidi wenye mishahara ya juu lakini huongeza zaidi pengo la mapato kati ya watumishi wa kada za juu na chini.


“Hali hii imefanya kuwepo kwa ubaguzi wa kimfumo, hivyo kuchochea kuibuka kwa matabaka na pengo baina ya walionacho na wasionacho, hivyo wakaitaka serikali kubadilisha utaratibu huo na ipandishe kwanza kima cha chini hadi sh. 315,000,”
alisema Bi. Suzan Lyimo ambaye aliwasilisha hotuba hiyo.


Aidha alisema kuwa ili serikali iongeze kiasi hicho cha mshahara, inatakiwa kupunguza posho na huduma za kuwalipia watumishi wa ngazi za juu kama huduma za maji, umeme, simu na zingine kwa kuwa hizi hazilipwi kwa watumishi wa ngazi ya chini.


“Tunaishauri serikali kupunguza misamaha ya kodi, kutumia vyanzo vya mapato vilivyoainishwa katika hotuba ya kambi hiyo, kuachana na matumizi yasiyo ya lazima ili iweze kupata fedha za kutosha zitakazowezesha kuongeza na kupandisha kima cha chini kwa mwaka huu wa fedha,” alisema Bi. Lyimo.


Bi. Lyimo pia alitumia mwanya huo, kuiomba serikali kupunguza kodi inayotozwa kwenye mishahara ya wafanyakazi ili waweze kubaki na fedha itakayowasaidia kutumia katika uchumi na kukuza uzalishaji.


Akizungumzia madai ya walimu, aliitaka serikali kutotumia vibaya uvumilivu wa walimu na badala yake iwalipe haraka madai yao.

0 comments

Post a Comment