Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - HABARI ZA KITAIFA , HABARI ZA LEO - Madaktari nchini wataka Waziri wa Afya na Naibu wake wajiuzulu

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
WAKATI madaktari wakisisitiza watagoma kesho kushinikiza kujiuzulu kwa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hadji Mponda na naibu wake, Dk Lucy Nkya, mawaziri hao jana walijifungia kwenye ofisi zao siku nzima, kuwakwepa waandishi wa habari.


Jana waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali nchini, walipiga kambi makao makuu ya wizara hiyo jijini Dar es Salaa kutaka kujua msimamo wa Dk Mponda na Dk Nkya, kuhusu madai hayo ya madaktari, lakini jitihada hizo ziligonga mwamba baada ya viongozi hao kujifungia ofisini tangu saa 3:00 asubuhi hadi saa 7:00 mchana waandishi walipoanza kuondoka.


Katika Ofisi ya Waziri Mponda, wanahabari walielezwa kuwa waziri hayuko tayari kuzungumzia suala hilo kwa sababu liko juu ya uwezo wake.


“Nataka mfahamu kuwa waziri anajua uwepo wenu, lakini hayuko tayari kuzungumza na waandishi wa habari, hawezi kuzungumzia suala hilo sababu lipo juu ya uwezo wake,” alisema Mmoja wa maofisa katika ofisi ya Waziri Mponda.


Pia katika Ofisi ya Dk Nkya waandishi walipoingia walikutana na mmoja wa wasaidizi ambaye alitoa kauli kama ya mtangulizi wake.Baada ya waandishi kusubiri kwa muda mrefu, ilipofika saa saba mchana, Ofisa katika Ofisi ya Waziri wa Afya, aliwaeleza kuwa angerudi tena ofisini kumshauri Waziri Mponda atoke ili aweze kuzungumza na wandishi hao.


Lakini, baada ya muda alitoka Msemaji wa Wizara hiyo aliyekuwa kwenye mkutano wa wakurugenzi wa Idara zote za Wizara ya Afya, Nsachris Mwamwaja na kusisitiza, kuwa mawaziri hawakuwa na cha kusema juu ya suala hilo kwani liko juu ya uwezo wao.“Suala la madaktari linajadiliwa katika ngazi za juu, mawaziri hawawezi kutoa maoni wala tamko lolote juu ya jambo hili,”alisisitiza Mwamwaja.


Msimamo wa madaktari
Jana, Rais wa chama cha Madaktari Tanzania (MAT), Dk Namala Mkopi alisisitiza msimamo wa madaktari hao waliootoa mwishoni mwa wiki kuwa watagoma kesho endapo mawaziri hao hawatakuwa wamejiuzulu.


“Madaktari walishapitisha hili kwenye kikao chao, msimamo wao ni ule ule kwamba wao hawataendelea kufanya kazi, ikiwa mawaziri hao watakuwa hawajajiuzulu ifikapo Jumatano (kesho).Mwishoni mwa wiki iliyopita madaktari walitoa tamko kumtaka Rais Jakaya Kikwete awawajibishe mawaziri hao vinginevyo, wataanza mgomo kesho.


Madaktari wanawatuhumu kuwa viongozi hao kuwa chanzo cha mgomo uliotangazwa Januari 23, ambao ulisababisha vifo vya watu kadhaa na wengine wengi kuathirika.Pamoja na msimamo huo wa madaktari hadi jana, mawaziri hao hawakuonyesha dalili yoyote ya kuwajibika wenyewe.


Wizarani hapakaliki
Msemaji huyo akisema hayo, jana ukumbi wa mikutano wa Wizara ya Afya hiyo ulitawaliwa na vikao vya muda mrefu vilivyohusisha wakurugenzi wote wa wizara hiyo.


Habari za ndani zinasema wakurugenzi hao walikutana kujadili sakata hilo na namna watakavyokabiliana na tisho la mgomo huo.“Wakurugenzi wote wa Idara za Wizara wapo ndani ya kikao na wananendelea na mkutano chini ya Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali Dk Dolnald Mbando, wanajadili suala la Madaktari, wanatafuta namna watakavyokabiliana na tishio la mgomo,” kilisema chanzo hicho.


Akizunguzia hilo Mwamaja alikiri kuwepo kwa kikao hicho, lakini akabainisha kuwa kilikuwa cha uongozi wa Wizara na walikuwa wakijadili masuala mbalimbali yanyohusu wizara hiyo na si mgomo wa madaktari.


“Nikweli kulikuwa na kikao hapa wizarani, hiki ni cha menejimenti walikutana kujadili mambo mbalimbali, lakini hayahusiani na mgogoro wa madaktari,” alisema Mwamaja.

0 comments

Post a Comment