Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - HABARI ZA LEO - Dk Slaa achafua hewa kwa Pinda

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter

KATIBU Mkuu wa Chadema, Dk Willibroad Slaa amechafua hali ya hewa katika Jimbo la Katavi lililopo Mkoa mpya wa Katavi ambalo Mbunge wake ni Waziri Mkuu, Mizengo Pinda baada ya kuwaambia wananchi kuwa: "Kiongozi huyo anafurahia anasa za uwaziri mkuu."Dk Slaa alifanya mikutano mitatu ya hadhara jimboni humo jana katika vijiji vya Majimoto, Mbende na Usevya, alikozaliwa Pinda ikiwa ni mfululizo wa maandamano na mikutano inayofanywa na chama hicho katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.

Alisema Pinda anatembelea magari yenye gharama kubwa ambayo thamani yake ni Sh500 milioni huku wasaidizi wake nao wakipanda yaliyo na thamani ya Sh200 milioni wakati wapiga kura wake wana hali ngumu ya maisha.

"Nikiangalia hali ya maisha yenu wananchi wa jimbo hili, Mkoa wa Rukwa na Katavi si haki ninyi kuendelea kuishi kwenye nyumba za udongo na nyasi wakati kodi zinafujwa kila kukicha kwa matumizi ya anasa ya Serikali hii," alisema Dk Slaa.

Dk Slaa alisema mbali na anasa hiyo, semina elekezi kwa mawaziri inayoendelea mkoani Dodoma imegharimu fedha nyingi na  kwamba iwapo serikali ingekuwa inawajali wananchi wake, ingeweza kujenga shule za sekondari katika jimbo zima la Waziri Mkuu kwa kutumia fedha zinazotumika katika semina hiyo.

"Leo Pinda na Rais Jakaya Kikwete wako Dodoma kwenye Semina Elekezi, wanatumia kodi za wananchi na baadaye wanarudi kuwakamua kwa kupandisha gharama za maisha na kutoza kodi kubwa," alisema.

"Kikwete amewateua mawaziri kisha anawaandalia semina za kazi gani? Kama hawana uwezo wa kuongoza si angeteua wabunge wengine? Alisema mawaziri walioshindwa kufanya kazi wajiondoe wenyewe. Kwani anajua mawaziri wake hawafai, lakini badala ya kuwafukuza anawapa ruksa wajiondoe wenyewe!"

"Pinda, kwa siku moja akiwa kule bungeni hupata posho ya Sh200,000 ambayo inazidi mshahara wa mwezi mmoja wa mwalimu, hata polisi anayelinda usalama wenu. Lakini magari anayotumia kwenye msafara wake yasiyopungua 30 gharama yake haipungui Sh600 bilioni. Gharama ya gari analotembelea mbunge wenu ni sawa na kujenga vituo vitano vya afya."

Dk Slaa aliyekuwa mgombea urais katika Uchaguzi Mkuu Oktoba mwaka jana alisema, inasikitisha kuona Mbunge wa Katavi anakuwa mbinafsi kwa kujiwekea umeme wa jua kwenye nyumba yake pekee katika Kijiji cha Usevya badala ya kuupeleka kwa wananchi wote.

"Inasikitisha kuona mbunge wenu anakuwa mbinafsi kwa kujiwekea umeme wa jua katika nyumba yake iliyopo Usevya badala ya kupeleka umeme ambao ungeweza kutumiwa na wananchi wote. Nyinyi wenyewe mnaona kwenye nyumba yake pale kuna umeme wa nguvu ya jua, wakati ninyi wapigakura wake mkiwa kwenye dimbwi la giza hamuoni kama ni ukatili mkubwa? aliuliza.

Zitto amjibu Waziri Mkulo
Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe alisema atamthibitishia bungeni, Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo kuwa Serikali imefilisika.Zitto alisema jana mjini Sumbawanga kuwa wataweka hadharani jinsi Serikali ilivyokopa fedha benki ili Waziri Mkulo aweze kuwajibika kutokana na kauli yake aliyoiita ya kukataa kusema ukweli.

Alisisitiza kwamba serikali haina fedha na kudokeza kuwa taarifa ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ya mapitio ya uchumi ya mwezi Machi mwaka huu, inaonyesha kuwa imeshindwa kukusanya kodi kwa asilimia 15.

"Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Serikali katika makusanyo ya kodi zote imeshindwa kukusanya kodi kwa asilimia 15 isipokuwa ushuru wa forodha. Hivyo haikufikia malengo ya ukusanyaji wa kodi," alisema Zitto.

Kwa mujibu wa Zitto, Machi, mwaka huu Serikali ilikopa fedha katika Benki ya Exim na benki zote za biashara nchini na ilikuwa ikihangaika ili iweze kuwalipa wafanyakazi.

"Mkulo atueleze ni serikali gani duniani inakopa kwenye benki za biashara kwa kuwa kitendo hicho ni hatari sana kwa nchi," alisema na kuongeza:"Bajeti ya mwaka uliopita ilikuwa ni Sh11 trilioni ambayo Serikali ilishindwa kufikia malengo ya Sh 1.6 trilioni kutokana na kushindwa kukusanya kodi kwa asilimia hiyo 15 isipokuwa ushuru wa forodha."
Alimtaka Mkulo kuacha kuwaona wanaosema kwamba serikali haina fedha si wazalendo kwa kuwa wawekezaji hawatakuja nchini, bali atambue kuwa kukosekana kwa fedha si suala la uzalendo.

"Serikali ni kweli haina fedha na hakuna suala la uzalendo katika hili. Tatizo la uwekezaji ambalo analizungumzia, linatokana na sera mbovu za CCM kwa kuwa tangu mwaka 2007, hakuna uwekezaji wowote wa maana uliofanyika hapa nchini," alisema Zitto.

Akiwahutubia wanachama wa Chadema na wananchi wa mji wa Vwawa, Mbozi, mkoani Mbeya hivi karibuni, Zitto alisema Serikali ina hali mbaya kifedha kwa sasa kiasi cha kukopa ili kulipa mishahara ya wafanyakazi.
Alidai kuwa hali hiyo mbaya kifedha kwa serikali imesababisha watumishi wake pamoja na wabunge kutolipwa mishahara hadi Mei 7, 2011.

Alisema Serikali sasa inatafuta fedha za kuwalipa watumishi wake mishahara ya mwezi Aprili.
"Hata sehemu ya posho za wabunge mkutano uliopita, zikiwemo za kugharimia mafuta ya safari za wabunge majimboni bado hazijalipwa kutokana na Serikali kukosa fedha," alidai Zitto.

Alisema kutokana na hali hiyo, Serikali imekwenda kukopa Sh540 bilioni kutoka benki za ndani ili watu wasijue kuwa inakabiliwa na ukata."Serikali haikopi fedha ili ijenge bandari, viwanda au kugharimia miradi ya maendeleo, bali inakopa ili ilipe mishahara ya wafanyakazi," alisema Zitto.

0 comments

Post a Comment