Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - HABARI ZA LEO - Mafisadi CCM 'kushughulikiwa'

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
KATIBU wa Itikadi na Siasa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye amesema chama hicho kitaanza kuwashughulikia vigogo wake waliojibinafsishia baadhi ya miradi ya chama kwa maslahi yao.

Nnauye amesema,vigogo hao wamekuwa wakitafuna kama mchwa fedha zinazopatikana kwenye miradi hiyo na hakuna hatua zozote dhidi yao zilizochukuliwa.

“Kwenye miradi yetu ya CCM nako kuna ufisadi kweli, kuna mahali fulani kiongozi amesaini mkataba wa zaidi ya miaka 200 na wawekezaji, unaweza ukaona mwenyewe mkataba huo ulivyo wa kifisadi na watu wako kimya,” alisema bila kumtaja kiongozi huyo na sehemu ulipo mradi huo.

Akizungumza na wanahabari mjini hapa hivi karibuni, Nnauye alisema CCM ina miradi yenye thamani ya jumla ya Sh bilioni 50 nchini.

Alisema, Operesheni Vua Gamba inayoendelea ndani ya chama hicho, itahusu pia wasimamizi wa miradi hiyo na watakaobainika kuihujumu, watavuliwa nyadhifa na kuchukuliwa hatua kisheria.

“Tunahitaji kujiimarisha kiuchumi na ili tuweze kufanikiwa, ni lazima kuwe na udhibiti wa kutosha wa mapato yatokanayo na miradi yetu, badala ya kuacha baadhi ya viongozi kuiendesha kama mali yao,” alisema.

Alisema, katika maeneo mengi taarifa za mapato na matumizi ya fedha zitokanazo na miradi ya chama, imekuwa haieleweki vya kutosha na akashangaa hali hiyo kufumbiwa macho. Nnauye alisema pia kwamba katika mkakati wake wa kujivua gamba, chama hicho hakitasubiri ushahidi wa vyombo vya Dola.

“Kushughulikia mafisadi ndani ya chama hatutasubiri ushahidi wa vyombo vya Dola, tutawalazimisha wanaotajwatajwa kuachia ngazi bila kujali kama vyombo hivyo vinafanya kazi au la,” alisema.

Alipoulizwa kama kelele zake dhidi ya mafisadi ndani ya chama hicho zinahusishwa na mikakati ya kujitengenezea njia ili atakapokidhi sifa zote, awanie urais, Nnauye alisema hata siku moja hajawahi kufikiria hivyo.

“Niseme ukweli wangu wa moyoni, sijawahi kuwa na ndoto ya kuwania urais, wala sina mtu ninayempigia debe, kazi ninayofanya mimi ni kwa maagizo ya chama changu kwa kuzingatia mkakati tulionao wa kujisafisha,” alisema.

Wakati huo huo, Kanisa la Assemblies of God kupitia kwa aliyejitambulisha kama Askofu Mwalyego, limewataka watakaothibitika kuwa mafisadi, wawajibike kwa kufanya toba inayoambatana na malipizo ya mali walizoiba.

Katika taarifa yake kwa umma juzi, Kanisa hilo lilisema wapo watu waliolifikisha Taifa hapa lilipo sasa, na kuna ulazima wa watu kuwa wakweli na kuepuka woga wa kulindana ili kulinusuru Taifa.

“Wapo watu waliolifikisha Taifa hapa lilipo na wanapaswa kuwajibika mbele za Mungu na wanadamu … kama kila kiongozi wa dini ataamua kumlinda mwumini wake, basi Taifa litaingia katika udini na amani itatoweka,” alitanabaisha Askofu Mwalego. Alipongeza na kuwaombea kwa Mungu awape ujasiri waliodhamiria kufichua mafisadi na kuwatupa nje.

“Nawaomba viongozi wenzangu wa dini kutenga muda na kumwombea Rais Jakaya Kikwete aendelee na kazi aliyoianza na hatimaye kuwamaliza mafisadi, kwani mara zote kazi ya Mungu huwa inakabiliwa na upinzani mkubwa wa shetani kama ilivyoanza kujibainisha,” alisema Askofu huyo.

Alisema, hivi sasa wameanza kujitokeza baadhi ya viongozi wa dini kupinga hatua zinazochukuliwa na CCM chini ya operesheni yake ya kujivua gamba, kwamba ni kujing’oa vibanzi na kuacha vigogo machoni mwao.

“Kauli kama hizi zinapotosha na kupingana na maandiko, ambapo mpango wa Mungu ambao Wakristo nchini tumekuwa tukiuomba ni mafisadi wote kuwajibika,” aliongeza Askofu Mwalego.

0 comments

Post a Comment