Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Ugunduzi: Mkojo kutumiwa badala ya petroli, dizeli

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
WAKATI dunia ikishuhudia kupanda kwa bei ya mafuta, wanasanyansi wamegundua kuwa mkojo wa binadamu unaweza kutumika kama nishati ya kuendeshea magari badala petroli na dizeli.

Taarifa iliyotolewa kwenye tovuti ya Asasi ya Kimataifa ya Teknolojia ya Mazingira (IET), Machi 10, mwaka huu iliripoti juu ya wanasayansi wa Uingereza kugundua namna ya kutumia mikojo kuendesha injini za magari.

Ugunduzi huo mpya unaweza kupunguza gharama kubwa zinazotumika sasa kununulia petroli, dizeli na gesi duniani kuendeshea mitambo pamoja na kupunguza uchafuzi wa mazingira kutokana na matumizi ya mafuta.

Ugunduzi huo unaweza pia kupunguza kuyumba kwa uchumi duniani kutokana na nchi zinazozalisha mafuta kupunguza uzalishaji nishati hiyo hivyo kusababisha kupanda kwa bei mara kwa mara.

Wanasanyansi hao wanasema mkojo unaweza kutumika badala ya nishati hizo ambazo zimezoeleka ulimwenguni kwa sasa. Tayari wataalamu nchini humo wamebuni njia ambazo zitatumika kukusanya na kuvuna mkojo wa binadamu ili uanze kutumika kama nishati.

Wanasayansi hao wa Uingereza wamegundua teknolojia hiyo kwa kutumia matokeo ya utafiti wa Profesa Gerardine Botte wa Chuo Kikuu cha Uhio, Marekani aliyeufumbua macho ulimwengu juu ya namna ya kuzalisha nishati kwa kutumia mkojo.

Katika ugunduzi huo alioutangaza mwaka 2009, Profesa Botte alielezea jinsi ya kupata nguvu ya nishati kwa teknolojia ya kutumia ya haidrojeni kwenye mkojo.

"Kinachofanyika hapa ni kutumia teknolojia ya kuzalisha nguvu ya hydrojeni kutoka kwenye mkojo," gazeti la The Guardian la Uingereza lilimnukuu Profesa Gotte.

Alitoa mfano kwamba ng'ombe 1,000 wakikojoa kwa wakati mmoja wanaweza kuzalisha nguvu ya nishati ya kilowati kati ya 40 hadi 50 na kuwa mitandao mingine na pia katika maeneo ya kazi yenye watu 200 hadi 300 wanaweza kuzalisha kilowati mbili.

Aliuelezea ugunduzi wake kuwa ni wa muhimu kwa sababu binadamu atapata nishati nyingine rahisi na pili, matumizi hayo yatapunguza kiwango cha kemikali za amonia ambazo zinatupwa kwenye ardhi, jambo ambalo ni uharibifu wa mazingira.

Wanasayansi hao wa Uingereza waliofanyia uchunguzi ugunduzi wa Profesa Botte nao wamekuja na hatua ya kwanza ya kutumia mkojo kwa matumizi ya kuendesha injini za magari badala ya petroli, dizeli au gesi asilia.

Wanasayansi hao baada ya kuona mkojo ni njia muafaka ya kupata nishati, waliainisha baadhi ya vyanzo vikuu vya kupata mkojo.

Walipendekeza maeneo ambayo yanaweza kutumika kwa ajili ya uvunaji wa mkojo kuwa ni vituo vikuu (stendi) vya mabasi, viwanja vya michezo hasa mpira wa miguu na maeneo mengine ambayo yanakuwa na mikusanyiko mikubwa ya watu kama vile masoko na maeneo ya mijini.

Tayari mamlaka za miji Uingereza zimepewa taarifa za kitaalamu ili kubadilisha mifumo ya usafirishaji wa majitaka na kuweka mazingira mazuri ya kuvuna mkojo.

Kwa mujibu wa wataalamu hao mfumo huo ni pamoja na kuwezesha kutengenisha njia kusafirisha mkojo na kinyesi.

Mmoja wa wanasayansi waliofanyia uchunguzi ugunduzi wa Profesa Botte ni Sarah DeWeerdt ambaye aliandika taarifa akimsifu kuwa ameleta mapinduzi ya nishati duniani.

Sarah alielezea kuwa kinachofanyika kwenye ugunduzi huo ni kuzalisha nishati ya haidrojeni kwa kutumia mkojo ambayo inaweza kutumika kwenye magari na mitambo mingine.

Wanasayansi wengine walisema pia matumizi ya mkojo yatapunguza utegemezi wa mafuta yanayochimbwa ardhini hasa ikizingatiwa kuwa urasimu wa wazalishaji unayumbisha uchumi katika nchi nyingi duniani.

Uzalishaji wa mafuta
Kiwango kikubwa cha mafuta yanayotumika duniani hutoka katika nchi za Kiarabu na ndizo zenye nguvu kubwa ya kupanga bei ya nishati hiyo kupitia Umoja wao unaojulikana kwa kifupi OPEC.

Gharama za maisha zimepanda kwa kiasi kikubwa nchini hali ambayo Rais Jakaya Kikwete alisema imechangiwa na kupanda kwa bei ya mafuta katika soko la dunia.

Wachunguzi wa mambo wanasema kama teknolojia hiyo ikifanikiwa na kuanza kutumika inaweza kuwa mkombozi wa kiuchumi.
Tags:

0 comments

Post a Comment