Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Mawakili kupinga uteuzi wa Jaji Mkuu Zanzibar mahakamani

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
CHAMA cha Mawakili Zanzibar (ZLS) kinatarajia kuishtaki Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), kikipinga Jaji Mkuu Zanzibar, Hamid Mahmoud Hamid kuendelea na wadhifa huo kwa madai kwamba uteuzi wake una shaka kikatiba na ulikiuka taratibu za kisheria.

Taarifa iliyotumwa jana kwa gazeti hili na kusainiwa na Rais wa ZLS, Yahya Khamis Hamad imesema uamuzi huo ulifikiwa Februari12, mwaka huu na mkutano mkuu chama hicho.

“TLS imechukua hatua hii kutokana na kuamini kuwa uteuzi wa Jaji Hamid Mahmoud kuwa Jaji Mkuu wa Zanzibar una mashaka tele ya kikatiba. Inaeleweka kwamba Hamid Mahmoud alistaafu kwa hiari alipotimiza miaka 60. Baada ya hapo, Kikatiba, alisita kuwa Jaji Mkuu na Jaji wa Mahakama Kuu," imeeleza taarifa hiyo na kuongeza:

"Iwapo alitakiwa kuendelea kushika wadhifa huo, alipaswa kwanza kupewa mkataba wa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu. Mkataba wa aina hiyo ulilazimu kujadiliwa na Tume ya Utumishi ya Mahakama kwa mujibu wa kifungu cha 95 (1) cha Katiba ambacho kinasema; Bila ya kuathiri masharti ya kifungu hiki, Jaji wa Mahakama Kuu ataendelea kushika wadhifa wake hadi kufikia umri wa miaka 60 ambapo anaweza kustaafu kwa hiari ama kuendelea hadi kufikia umri wa miaka 65 ambapo atastaafu kwa lazima."

"Aidha (2) Bila ya kuathiri masharti ya kifungu cha (1) cha kifungu hiki, Rais kwa kushauriana na Tume ya Utumishi ya Mahakama anaweza kumteua tena Jaji aliyekwishastaafu kushika madaraka ya Jaji wa Mahakama Kuu kwa muda au kwa ajili ya kesi maalumu."

Kutokana na maelezo hayo, ZLS imesema kuwa hakukuwa na sababu yoyote kwa Jaji Mkuu huyo kuendelea kufanya kazi katika mkataba kwa kuwa Katiba ilikuwa inamruhusu kuendelea na ajira hadi kufikia miaka 65.

Ilisema kuwa iwapo Jaji Mkuu alitakiwa kuendelea na nafasi yake baada ya kumaliza utumishi wake, ililazimu mambo mbalimbali kufuatwa kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar (kifungu cha 94(1), 94(2), 94(6)(a) na (b).

Imeyataja mambo hayo kuwa ni pamoja na kuwa ateuliwe kwanza kuwa Jaji wa Mahakama Kuu; Mapendekezo ya (a) yatokane na Tume ya Utumishi ya Mahakama; Endapo ni Jaji wa Mkataba: “Masharti ya kazi, marupurupu na kiinua mgongo cha jaji wa mkataba wa kipindi maalumu yataamuliwa na Tume ya Utumishi ya Mahakama.” (Kif.94(6)(b), Iwapo atateuliwa kuwa Jaji basi atakula kiapo cha Jaji wa Mahakama Kuu.

“Kuendelea kwake kuwa Jaji Mkuu kunakuwa na mashaka ya kikatiba na sisi tusingependa nchi yetu iwe na Jaji Mkuu ambaye uteuzi wake umegubikwa na kasoro kadhaa za kikatiba,” ilieleza ZLS.
 
Kwa mujibu wa ZLS, suala la kuwa Jaji au Jaji Mkuu wa mkataba linapigwa vita katika Mahakama za Jumuiya ya Madola kwa sababu mikataba inaondoa kinga ya kikatiba aliyonayo Jaji wa Mahakama Kuu, hivyo kudumaza uhuru wa Mahakama na kwamba Jaji wa mkataba hawezi kufanya kazi yake bila ya hofu wala woga kwa mamlaka ya uteuzi.

Hata hivyo, ZLS ilisema kuwa haihoji mamlaka ya Rais kikatiba, bali inatoa mchango wake katika kujenga mahakama iliyotukuka, hasa kutokana na wananchi kupoteza imani kwa mahakama zilizopo sasa.

Desemba mwaka jana, ZLS ilipinga uteuzi wa Majaji wa Mahakama Kuu uliofanywa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Ali Mohammed Shein Novemba 29 na kwamba hakikuridhishwa na uteuzi huo kwa kuwa haukuzingatia vigezo na ulikiuka sheria kwa kuwa hakikushirikishwa.

Rais wa Zanzibar kwa mamlaka aliyopewa, alifanya uteuzi wa majaji wanne wa Mahakama Kuu, Abdul-hakim Ameir Issa, Fatma Hamid Mahmoud, Mkusa Isaac Sepetu na Rabia Hussein Mohammed pamoja na Mwenyekiti wa Mahakama ya Ardhi, Haroub Sheikh Pandu. ZLS kilisema hakina shaka na uteuzi wa Issa wala Pandu, bali hao wengine.
Tags:

0 comments

Post a Comment