Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Wanafunzi UDOM Wamteka mkuu wa Wilaya

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter

MGOMO wa wanafunzi na Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) umechukua sura mpya baada ya wanachuo hao kumteka na kumweka chini ya ulinzi kwa saa manne Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, John Tupa, wakitaka wamuone Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.Tukio hili la aina yake lilitokea jana mchana na kuvuruga hali ya usalama katika eneo hilo hivyo kumlazimisha Pinda ambaye alikuwa akifanya mazungumzo na menejimenti ya chuo hicho kuondoka kupitia njia nyingine akiwa chini ya ulinzi mkali.

Tupa aliingia katika mikono ya wanafunzi saa saba mchana katika eneo Chimwaga alipoenda chuoni hapo kufanya maandalizi ya kumpokea Waziri Mkuu Pinda ambaye wakati huo alikuwa kwenye kikoa na uongozi wa chuo katika jengo la utawala lililopo umbali unaokadiriwa kuwa kilomita mbili.

Kwa mujibu wa watu walioshuhudia tukio hilo, baada wanafunzi kulizingira gari la DC Tupa walitoa upepo kwenye matairi yote ya gari lake huku wakipaza sauti kuwa hawatamwachia mpaka Waziri Mkuu Pinda afike katika eneo hilo.

Kundi hilo la wanafunzi ambalo lilikuwa likitoa vitisho kwa Tupa lilimfanya dereva wake ambaye alifanikiwa kutoka kwenye gari kukumbia na kumuacha bosi wake akiwa chini ya ulinzi wa wanachuo hao.


Awali, Pinda alipowasili chuoni hapo alipokelewa kwa shangwa na umati mkubwa wa wanafunzi wakiwa pamoja na wahadhiri.

Pinda alishuka kwenye gari lake na kusalimiana nao huku wakipiga kelele "Tunataka, haki zetu!" lakini hakuzungumza chochote na akapanda kwenye gari lake kuelekea kwenye jingo la utawala ambako alikutana na menejimenti na viongozi wa serikali ya wanafunzi.

Wakati Pinda anaondoka, umati mkubwa wa wanafunzi ulifanya jaribio la kumzuia ili waanze kumueleza kero zao, lakini walishindwa baada ya msafara kupenya na kuondoka.

Hali hiyo ilielekea kuwaudhi na mkuu huyo wa wilaya alipowasili kwenye eneo hilo kuandaa mapokezi, wakamgeuzia hasira zao na kumteka wakidai hawatamuachia hadi Pinda afike kuzungumza nao.

Kufuatia hali kuwa tete, baada ya  kumaliza mazungumzo na uongozi wa chuo Pinda aliondoka saa 12.30 jioni chuoni hapo kwa kupitia kitivo cha sayansi ya jamii ambacho kimemaliza mgomo akiwa na ulinzi mkali na kuwaacha wanafunzi wa kitivo cha elimu na wahadhairi wao wakimsubiri.


Msafara wa Pinda ulioondoka chuoni hapo bila kingora cha polisi, jambo ambalo si la kawaida kiongozi huyo anaposafiri kwa kutumia magari.

Baada ya kumkosa Pinda wanachuo waliamua kumwachia Tupa, ambaye alitafuta usafiri mwingine kutokana na matairi ya gari lake kutokuwa na upepo.

Mwanachi Jumapili ilipowasiliana naye kwa njia ya simu mara baada ya kuachiwa, Tupa alisema hangeweza kulizungumzia tukio hilo badala yake litatolewa ufafanuzi na kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma leo.


Wanafunzi wa Udom wamekuwa kwenye mgogoro na serikali tangu mwishoni wa mwaka jana ambapo wanachuo wa kitivo cha Sayansi ya Jamii waliandamana kabla ya mwanzoni mwa wiki hii kitivo cha elimu pamoja na wahadhiri nao kuanzisha mgomo wakilalamikia kupunjwa mishahara.

Tukio hilo ambao lilionekana kama ni sinena, lilizua tafrani kubwa miongoni mwa wapita njia na wakazi wa eneo hilo baada ya wanachuo kufunga barabara na kuzuia wapita njia wote wakisema wanahitaji kuona gari ambalo litakuwa limembeba Waziri Mkuu na si vinginevyo.

Polisi wakiwa na silaha na mabomu ya machozi walilizingira eneo hilo na wakashindwa kuwamwokoa Tupa wakihofia kuchafua hali ya usalama chuoni hapo.


Wakati wanafunzi hao wamemdhibiti Tupa walisikika wakisema, "Hatoki mtu hapa mpaka kieleweka". Baadhi ya wanafunzi walisikika wakiimba kwa sauti za juu huku wengine wakiwaonya polisi wakijaribu kuwashambulia watakufa na mkuu wa wilaya huyo. 

Mwandishi wa gazeti hili ambaye alifika katika eneo hilo saa nane mchana alishuhudia gari la mkuu huyo wa wilaya likiwa chini ya ulinzi wa wanachuo wenye hasira huku askari polisi wengi wakiwa wamezunguka eneo hilo kwa mbali wakizuia watu wengine kuwasogelea.

Mmoja wa polisi hao aliliambia Mwananchi Jumapili kwamba walipogundua kuwa wanafunzi wametoa upepo gari la Mkuu wa Wilaya waliona bora wawe na utulivu baada ya kuwahakikishia kuwa  hawatamduru.

"Tunaona tukiingilia kati, tunaweza tukazusha vurugu, hivyo ni vema kutumia busara maadamu wameahidi kutomduru," alisema polisi huyo kwa sharti la kutotajwa jina lake gazetini kwa sababu siyo msemaji wa jeshi hilo.

Hii ni mara ya pili kwa Tupa kutekwa na wanachuo hao, mara ya kwanza ilikuwa katika mgomo wa Januari 10, mwaka huu mara alipomaliza kuzungumza nao katika Viwanja vya Bustani ya Mwalimu Nyerere wakimlazimisha awasindikize ili iwe ni kinga yao dhidi ya kupigwa mabomu na polisi.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Zelothe Stephen, alipopigiwa simu yake ya mkononi hakuipokea hivyo kusababisha wasiwasi kwamba huenda mkuu wa walaya yuko kwenye wakati mgumu kwani hata yeye alikuwa hapokei simu.


Wakati huo huo wahadhiri ambao walianzisha mgomo kwa zaidi ya wiki moja sasa walikuwa wakimsubiri katika ukumbi wa Chimwaga Waziri Mkuu ili aweze kuzungumza nao na walisema kuwa wako tayari kumsikiliza hata kama ni usiku wa manane.

Baada ya wanafunzi hao kupata taarifa kwamba Pinda ameondoka na ameahidi kukutana nao leo saa tatu, walimuachia huru mkuu huyo wa wilaya wakidai wanaenda kujiopanga kuzungumzia juu ya kiongozi huyo waliyemsubiri kwa hamu kuwakwepa.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Uongozi wa Chuo hicho kupitia kwa makamu Mkuu wa Chuo Profsa Idrisa Kikula, Pinda alitarajia kuwasili jana majira ya mchana kisha kukutana na wanachuo kwa ajili ya kusikiliza kero zao.

Kero kubwa kwa wanachuo hao ni pamoja na mazingira mabovu ya kusomea, ukosefu wa vifaa, wahadhiri wasio na sifa pamoja na ukosefu wa maji kwa muda mrefu ingawa tatizo hilo juzi lilionekana kupatiwa ufumbuzi baada ya Mamlaka ya Maji safi na Maji Taka mjini Dodoma (Duwasa) kutengeneza miundombinu na hali kurudia kuwa ya kawaida.


Sent from my iPhone
Tags:

0 comments

Post a Comment