Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Nahodha akerwa na tozo la mil 5/- kuzima moto

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
TAFRANI KIKAONI! Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya ulinzi ya Knight Support, David Sutton akitishia kuondoka kikaoni kwa ghadhabu baada ya Kamishna Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Jenerali Matwani Kapamba (kushoto) kumueleza Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Shamsi Vuai Nahodha (wa pili kulia) kuhusu kampuni yake, wakati waziri huyo alipotembelea kampuni hiyo ikiwa ni sehemu yake ya ziara kwa kampuni mbalimbali binafsi za ulinzi na uokoaji, Dar es Salaam.




WAZIRI wa Mambo ya Ndani, Shamsi Vuai Nahodha amekerwa na tozo la Sh milioni tano linalotozwa na Kampuni ya Ulinzi ya Knight Support kwa ajili ya kupata huduma ya zimamoto, akisema kampuni hiyo haijali maslahi ya jamii, na kutaka mabadiliko ya sheria ili kurekebisha hali hiyo.

Nahodha alionesha kukerwa huko katika ziara yake jana aliyokuwa akitembelea kampuni binafsi za ulinzi na uokoaji Dar es Salaam, na alishangaa kuona kuwa baadhi ya matakwa ya
kisheria hayatekelezwi na baadhi ya kampuni hutoza Sh milioni saba (Dola za Marekani 5,000) katika tukio la moto.

Moja ya kampuni hizo ni Knight Support ya Uingereza, ambayo jana baada ya kubanwa na maofisa wa serikali waliofuatana na Nahodha, Mkurugenzi Mkuu wake, David Sutton alitaka kuondoka mkutanoni kutokana na kubanwa na maswali yaliyomtaka afafanue gharama hizo.

Tafrani ilizuka baada ya Kamishna Mkuu wa Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji nchini, Matwani Kapama kueleza kuwa wamekuwa na ushirikiano mzuri na kampuni hizo, lakini baadhi yamekuwa yakitoza fedha kwanza kabla ya kutoa huduma hasa za kijamii inapotokea tatizo, ikiwemo Knight Support.

“Unasema uongo wewe, si kweli kwamba hatutoi huduma bali tunadai pesa kwanza, tumekuwepo kwenye matukio kadhaa nashangaa kusikia leo unasema haya,” alimaka Sutton huku akisimama akiashiria kuondoka eneo la kikao kwa hasira, lakini baadaye alirejea na kukaa kwa mazungumzo zaidi.

Wakati wa rabsha hiyo, Waziri Nahodha alikuwa radhi Mkurugenzi huyo aondoke na kusisitiza kuwa anatambua kuwa wanafanya biashara na anawaruhusu waendelee, lakini aliwataka kuhakikisha kuwa Mtanzania wa kawaida hakosi huduma linapotokea tatizo kwa sababu ya kushindwa kulipia.

“Natambua kuwa mpo hapa kama wawekezaji wengine na mnafanya biashara, sina shida na hilo, je mnawasaidiaje hao wananchi wa kawaida ambao hawana uwezo wa kulipa shilingi milioni tano na zaidi?

Serikali ifanye nini kuwawezesha nyie mtekeleze hilo,” alisema Nahodha na kuongeza: “Nakuagiza Kamishna (Kapama) mkae wiki hii na kampuni hii muangalie matakwa ya leseni, sheria na sera ili kuona namna mwananchi anapata huduma, tupo kutumikia Watanzania kwanza.”

Akifafanua kuhusu ushiriki wa kampuni hiyo katika majanga ya moto na uokoaji hasa ya kijamii, Kamishna Kapama alitolea mfano wa tukio la Ubungo katika matangi ya mafuta ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) yaliyolipuka mwaka 2003 kuwa kampuni hiyo iliweka
kambi makao makuu ya Tanesco badala ya eneo la tukio Ubungo Maziwa.

Nahodha aliitaka kampuni hiyo kuona haiwatendei haki wananchi kwa kulipa ada ya leseni ya Sh 500,000 kwa mwaka huku ikiwatoza watu Sh milioni tano kwa tukio la moto na kumuagiza Kamishna wa Kikosi cha Zimamoto kukaa na uongozi wa kampuni hiyo kuainisha huduma kwa jamii.

Awali, akiwa katika Kampuni ya Ultimate, Nahodha aliipongeza kampuni hiyo kwa kushiriki kikamilifu katika matukio ya moto na uokoaji ya kijamii kama wakati wa milipuko ya mabomu Mbagala, bila kudai malipo na kuongeza kuwa kiwango cha tozo la Sh 15,000 mpaka 100,000 kwa tukio la moto si kibaya.

Alisema ili kuongeza uwajibikaji atawaandikia barua ya kuwapongeza kwa kazi nzuri na kueleza kuwa serikali inajiandaa kujenga vituo saba vya zimamoto katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam kwa hatua za mwanzo ili kuongeza nguvu na ufanisi katika kunusuru majanga ya moto.
Tags:

0 comments

Post a Comment