Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Arusha yapata meya wawili • ALIYEPEWA UNAIBU MEYA AWAGEUKA CCM

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter SAKATA la uchaguzi wa Meya wa Arusha mjini limeingia katika sura mpya baada ya mkurugenzi wa manispaa ya Arusha Estomii Chang’a kusema uchaguzi uliofanywa na kumshirikisha mbunge wa Viti Maalumu mkoa wa Tanga Mary Chatanda ulikuwa na baraka za Kaimu Katibu wa Bunge Eliakimu P. Mrema.
Chang’a alitoa ufafanuzi huo kwa waandishi wa habari jana wakati akijibu maswali ya waandishi kuhusiana na utata uliojitokeza kuhusu uchaguzi huo ambapo ilipelekea vurugu baada ya kutangazwa meya bila madiwani wa CHADEMA kuwepo.
Katika vurugu hizo mbunge wa jimbo la Arusha mjini, Godbles Lema alikamatwa na polisi kwa kichapo na kuswekwa rumande kwa saa kadhaa kabla ya kuachiwa na kulazimika kukimbizwa hospitali baada ya kuishiwa nguvu.
Akiongelea matukio hayo Mkurugenzi huyo alisema kufuatia utata uliojitokeza wa uhalali wa Mary Chatanda kupiga kura manispaa ya Arusha badala ya Tanga, alilazimika kuwasiliana na ofisi ya bunge kupata ufafanuzi ndipo alipoletewa barua iliyosainiwa na Mrema ikimhalalisha Chatanda kushiriki uchaguzi huo.
Alifafanua licha ya kupata ufafanuzi huo siku ya Ijumaa alilazimika kuahirisha kikao hicho cha baraza na kufanya kikao cha siri cha ndani siku ya Jumamosi ambapo madiwani wa CHADEMA hawakuhudhuria ndipo akalazimika kuendelea na taratibu za uchaguzi na kumtangaza Gaudensi Limo kuwa meya huku Michael Kivuyo akimtangaza kuwa ndie naibu meya.
Wakati mkurugenzi akitoa ufafanuzi huo aliyetangazwa kuwa Naibu Meya Michael Kivuyo (TLP) ameongea na waandishi wa habari jana na kusema uchaguzi uliofanyika haukuwa halali kwa kuwa ulikiuka baadhi ya kanuni za halmashauri.
Kivuyo alisema licha ya yeye kuchaguliwa kuwa naibu meya lakini atashirikiana na madiwani wa CHADEMA kupinga uchaguzi huo kwani ulikiuka taratibu mbalimbali za kikanuni za halmashauri.
Alipoulizwa kuhusu wadhifa wake kama ataendelea kuwa nao wakati anapinga uchaguzi huo alisema anawasiliana na chama chake ili atoe tamko la kujiuzulu nafasi hiyo ya unaibu meya kwa kuwa uchaguzi uliomchagua haukuwa halali.
Wakati hayo yakiendelea, madiwani wa CHADEMA hadi jana jioni walikuwa wanaendelea na kikao cha kumchagua meya wa jiji la Arusha ambapo nafasi hiyo ilikuwa ikiwaniwa na diwani wa kata ya Kimandolu Estomii Mala.
Akiongea na Tanzania Daima msemaji wa madiwani wa CHADEMA John Bayo alisema kuwa wao wanachagua meya wao na leo watamsindikiza katika ofisi za manispaa ya Arusha kuanza kazi za umeya.
Hali hiyo inamaanisha kuwa kutakuwa na mameya wawili katika ofisi moja hali ambayo si ya kawaida kutokea katika historia ya siasa za nchi hii.
Kwa hali hiyo, kinachotokea Arusha katika ngazi ya umeya kinafafana kabisa na kile kilichojitokeza nchini Ivory Coast ambapo nchi hiyo sasa inaongozwa na marais wawili baada ya kila moja kujitangaza rais.
Uchaguzi huo wa kumpata Meya wa jiji la Arusha uliingia tafrani kutokana na vyama vya CCM na CHADEMA kulumbana katika masuala ya kanuni, CHADEMA wakipinga mbunge wa viti maalum Mary Chatanda (CCM) kuwa mjumbe wa mkutano huo huku CCM nao wakipinga mbunge wa viti maalumu wa Rebecca Mgondo (CHADEMA) kuwa hajaapishwa kuwa mbunge hivyo hastahili kuwa mjumbe wa kikao hicho.
Wakati yote hayo yakiendelea, aliyetangazwa kuwa meya wa jiji la Arusha Gaudensi Lyimo (CCM), jana aliitisha kikao na waandishi wa habari chini ya ulinzi wa maofisa kadhaa wa polisi waliovalia kiraia, kuzungumzia yaliyojitokeza katika uchaguzi.
Kitendo hicho kiliwakera waandishi wa habari na kulazimika kumhoji Lyimo kwa kumtaka aeleze sababu za kuwaita askari kanzu hao katika kikao chake hicho kinyume na taratibu za kawaida za vikao kama hivyo vya wanahabari.
Katika majibu yake, Lyimo alijitetea kuwa wana usalama hao wamelazimika kuwepo kwa ajili ya kuangalia usalama wa eneo hilo kutokana na hali inayoendelea hivi sasa tangu kuvurugika kwa mkutano wa baraza la madiwani ambao yeye alitangazwa kuwa meya wa Arusha.
Majibu hayo hayakuweza kukidhi haja ya waandishi wa habari na kufikia hatua ya kulaumu halmashauri hiyo ya manispaa ya Arusha kuanza kutumia vyombo vya dola vibaya kitendo ambacho hata siku ya kikao cha baraza vilitumika kuwasambaza wananchi waliofika kutaka kusikiliza kikao hicho cha kwanza na kurushiwa mabomu ya machozi.
“Tunaomba tukwambie wazi kuwa kama ndio staili hii umeingia nayo, ofisini hii tutakuwa hatuji katika mikutano yako hata kama umetualika. Kutuletea askari ni kuingilia uhuru wa habari kwani tutakuwa tunashindwa hata kuuliza baadhi ya maswali kutokana na kukaa kwa hofu,” alisema Moses Mshala mwandishi wa habari wa gazeti la Mwananchi.
Aidha, akizungumzia suala hilo mwandishi wa habari wa gazeti la Raia Mwema, Paulo Sarwat, alisema kitendo cha polisi kuwafukuza waandishi katika kikao hicho cha baraza la madiwani ni cha udhalilishaji mkubwa kwa wanahabari na hali hiyo ikiendelea kuna hatari ya haki nyingi za wananchi kuhodhiwa bila maelezo ya msingi.
Baada ya malalamiko hayo ya waandishi dhidi ya udhalilishaji huo, ofisi ya mkurugenzi ililazimika kuomba radhi kwa kilichotokea na kuahidi hakitajirudia tena katika siku zijazo.
Tags:

0 comments

Post a Comment