Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - JK: Masauni kajimaliza mwenyewe

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter

Jakaya Kikwete
MWENYEKITI wa CCM Rais Jakaya Kikwete, amepiga msumari wa mwisho kwa aliyekuwa mwenyekiti wa UVCCM Hamad Yusuph Masauni, akisema alijimaliza mwenyewe kwa kutokuwa mkweli kuhusu umri wake na watu wasitafute mchawi.
 
*ADAI HATUA ALIYOCHUKULIWA KAMA YA NAPE, BENNO MALISA ASEMA NI USHUJAA KUWANG’OA VIGOGO
Leon Bahati, Iringa
 

Kauli hiyo ya mwenyekiti wa CCM taifa ilizidi kummaliza kijana huyo ambaye tayari alijikuta katika tuhuma nzito za kughushi umri ili achaguliwe mwaka 2008.  

Rais Kikwete aliweka bayana hilo mjini hapa wakati akifunga mkutano tete wa Baraza Kuu la UVCCM, ambao ulifanya vigogo wawili wa juu wote kutoka Tanzania Zanzibar, ambao ni Masauni na Naibu Katibu Mkuu Nassoro Moyo, kujiuzulu.

Mwenyekiti huyo wa CCM, awali katika hotuba yake hakutaka kuzungumzia kwa undani sakata hilo, lakini baada ya kumaliza aliruhusu maswali na ndipo baadaye akauliuza wajumbe:, "Hivi mlielezwa vizuri kilichomfanya Masauni ajiuzulu?"  

Baada ya swali hilo ukumbi ulipuka kwa wajumbe kusema:, "hatujuiii...hatujuiii...hatujuiii."

Jibu hilo lilimfanya Rais kuanza kufafanua kwa kifupi na kuwambia wajumbe:, " Kilichomponza Masauni ni kutokuwa mkweli kuhusu umri wake...Alikuwa na tuhuma za kughushi umri uliomwezesha kushinda uchaguzi mwaka 2008."

"Tulipochunguza ilibainika ni kweli alighushi, wakati wa uchaguzi alisema alizaliwa mwaka 1979, lakini ukweli alizaliwa mwaka 1973 na alianza darasa la kwanza mwaka 1979."

Rais Kikwete alisisitiza:, "Kwa hiyo hakuna aliyeonewa, aliyefitini na wala watu wasitafute mchawi katika hili. Hatua kama hii ilikwishafanyika kwa watu kama akina Nape (Nnauye)." Nape naye alienguliwa katika uchaguzi wa UVCCM uliopita.

Alisema taratibu za UVCCM mtu akishakuwa na umri wa zaidi ya miaka 31, hawezi kugombea nafasi kutaka kuchaguliwa kwani anakuwa amepoteza sifa inayohusika.

Mwenyekiti huyo wa CCM awali, aliwaonya vijana hao wa UVCCM kuacha magenge kwani watajimaliza wenyewe badala yake mambo yao yapatiwe ufumbuzi ndani ya vikao na taratibu za jumuiya na chama.

Mkuu huyo wa chama na nchi, alifafanua kwamba kama malalamiko yakipita katika njia na taratibu za chama ni rahisi kupatiwa ufumbuzi kuliko kuyaanika hadharani kama ilivyofanyika. 

Hata hivyo, Rais Kikwete alimfariji kijana huyo mpole na mzito kufanya maamuzi magumu na haraka, akisema kwakuwa ni makakamavu na mchapakazi atapangiwa kazi nyingine hapo baadaye.

Katika hatua nyingine, Rais Kikwete amewataka wana CCM kujiandaa kujibu mashambulizi ya wapinzani kuhusu tuhuma za ufisadi ambazo alisema anaamini, watazitumia kama mtaji wakati wa uchaguzi.

Awali, Makamu Mwenyekiti wa UVCC ambaye anakaimu nafasi ya Masauni, Benno Malisa, alisifia maamuzi ya kung'oka vigogo wenzake akisema ni ishara ya jumuiya kukomaa.

Malisa alitamba kwamba kitendo hicho kimeonyesha ushujaa ndani ya UVCCM na ni ishara ya ukomavu na ukuaji wa jumuiya.

Kwa wiki moja sasa, UVCCM walianza kurushiana makombora ya tuhuma nzito ambazo zilimtaja Masauni kwamba alighushi umri, taarifa ambazo zilisambazwa kwa njia ya waraka katika maeneo mbalimbali.

Gazeti hili ndilo la kwanza kuandika kuhusu wingu zito lililokuwa limetanda na kugubika mkutano huo wa vijana, huku duru zake zake za kisiasa za kuaminika, zikiweka bayana kwamba ilikuwa ni lazima kung'oka ama Moyo au Masauni au wote wawili, kitu ambacho kimetokea.
Tags:

0 comments

Post a Comment