Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Kiongozi wa zamani wa Panama apelekwa Ufaransa

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter

Kiongozi wa zamani wa Panama Mauel Antonio Noriega amewasili hatimaye nchini Ufaransa akikabiliwa na mashtaka ya kusafirisha fedha za madawa ya kulevywa.

 
Dikteta  wa  zamani  wa  Panama,  Manuel   Antonio Noriega,  amewasili  mjini  Paris  leo  baada  ya  Marekani kumhamishia huko  ili  afikishwe mahakamani  nchini Ufaransa   kwa  madai  ya  kusafirisha  fedha   za  biashara ya  madawa  ya  kulevywa  kinyume  na  sheria.
Ndege  ya  shirika  la   ndege  la  Ufaransa  iliyomchukua kiongozi  huyo  wa  zamani  wa  Panama,  mwenye  umri wa  miaka  74,  imewasili  katika  uwanja  wa  ndege  wa Charles de Gaulle  asubuhi  ya  leo  na  alipelekwa  moja kwa  moja  mahakamani   ili  kusikiliza   mashtaka   dhidi yake.
Kiongozi  huyo  wa  zamani   wa  Panama  aliondolewa kutoka  katika   jela mjini  Miami  jana  Jumatatu  ambako ametumikia  kifungo  cha  miaka  17  baada  ya kuondolewa  madarakani  mwaka  1989  wakati  rais  wa zamani  wa  Marekani,  George  Bush,  alipotuma   vikosi vya  jeshi  la  nchi  hiyo  nchini  Panama  kwenda kumkamata.
Noriega  amekuwa  kwa  muda  wa  miaka   kadha  akipinga kupelekwa  nchini  Ufaransa , ambako  katika  mwaka  1999 alihukumiwa  akiwa  hayuko  mahakamani  kwa  kusafirisha fedha  za  mapato  ya  biashara  ya  madawa  ya  kulevywa na  kuhukumiwa   kwenda  jela  kwa  muda  wa  miaka kumi.  Ufaransa  ilikubali  kufanya  kesi  hiyo  upya.
Noriega  alitakiwa  kufikishwa  mbele  ya  jaji    mahakamani mjini  Paris , ambaye  alitakiwa  kuamuru  kuwa  arejeshwe rumande  akisubiri   kufanyika  kesi  yake  ambayo  inaweza kuanza  kusikilizwa  katika  muda  wa  miezi  miwili, wamesema  maafisa  wa  Ufaransa.
Waziri  wa  mambo  ya   kigeni  wa  Marekani,  Hillary Clinton, alitia  saini  mjini  Washington hati  ya  kupelekwa Noriega  nchini  Ufaransa  jana  Jumatatu, na  kufikisha mwisho  miaka  kadha  ya  mvutano  wa  kisheria   kuhusu hali  ya  baadaye  ya  Noriega. Mawakili  wa  Noriega wanataka  aachiliwe  mara  moja, wakisema  kuwa kukamatwa  kwake  na  kupelekwa  nchini  Ufaransa  ni kinyume  na  sheria. 
Akiwa   kama  mtu  muhimu  sana  kwa  shirika  la  ujasusi la  Marekani, CIA,  hapo   zamani , Noriega  aliingia madarakani  nchini  Panama  akiwa   mkuu  wa  idara  ya upelelezi  katika   jeshi  la  nchi  hiyo  na  baadaye  kama mkuu  wa   jeshi  katika  miaka ya  80. Lakini  uhusiano wake  na  Marekani  uliharibika  kutokana  na  ripoti  kuwa amejiingiza   sana  katika  biashara  ya  madawa  ya kulevywa  na  kutiliwa  shaka  kuwa  alikuwa  pia akishirikiana  na  Cuba.
Desemba mwaka  1989, Bush  aliamuru  kukamatwa  kwa Noriega  ili  aweze  kufikishwa  mahakamani   nchini Marekani ,  na  kutuma  majeshi  nchini  Panama  katika operesheni  iliyopewa  jina  la  'kitendo  cha  haki'.
Baada  ya  Noriega  kukimbilia  katika   ubalozi  wa  Vatican mjini  Panama  City,  akiomba  hifadhi  humo, majeshi  ya Marekani  yalilizingira  jengo  hilo,  na  kupiga  muziki  kwa sauti  ya  juu  ili  kumfanya  ashindwe  kuvumilia. Siku kumi  za  mkwamo  zilimalizika  Januari  2 ,1990   wakati Noriega  alipojitokeza  nje  ya  jengo  hilo  la  ubalozi  na kujisalimisha kwa   majeshi  ya  Marekani  ambayo yalimsafirisha  hadi  Miami , jimboni  Florida  nchini Marekani. Alihukumiwa  kwa  makosa  ya   kufanya biashara  ya  madawa  ya  kulevywa  na  kusafirisha  fedha za  madawa  hayo na  kuhukumiwa  kifungo  cha  miaka  40 jela. Hukumu  hiyo  ilipunguzwa  na  kuwa  miaka  17 kutokana  na  kuwa  na  tabia  nzuri.
Tangu  wakati  huo  alibakia  katika  mamlaka  ya  serikali ya  Marekani  wakati  akipambana  dhidi  ya  ombi  la kupelekwa  nchini  Ufaransa.
Tags:

0 comments

Post a Comment