Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - HABARI ZA KITAIFA , HABARI ZA LEO - Wazamiaji 455 warejeshwa nchini

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
WATANZANIA 455 waliokuwa wamezamia katika nchi mbalimbali za kigeni, walirejeshwa nchini katika kipindi cha kati ya Januari na mwezi huu.Hayo yalisemwa jana na Kaimu Msemaji Mkuu wa Idara Uhamiaji, Tatu Burhan, alipokuwa akizungumza na gazeti hili ofisini kwake, jijini Dar es Salaam.




Burhan alisema vijana hao walirudishwa kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere na kwamba takwimu za vijana wengine waliorejeshwa kupitia viwanja vingine, hazijapatikana.Kaimu mkurugenzi huyo alisema hata hivyo kuna uwezekano kuwa idadi ya vijana waliorejeshwa nchini ni kubwa.


Alisema matukio ya mara kwa mara yanayohusu Watanzania na hasa vijana kuzamia meli kwa lengo la kwenda nje ya nchi na kufanya kazi, yameleta changamoto mpya, baada ya hivi karibuni baadhi ya Mashirika ya ndege kuanza kukataa kuwasafirisha wazamiaji hao kwa hofu ya kuzua fujo .


Alisema uchunguzi uliofanywa na Ubalozi wa Tanzania huko Beijing, China, umebaini kuwa Watanzania wawili walikataliwa kupanda ndege ya Shirika la Emirates kwa madai kuwa si sera ya shirika hio kusafirisha wazamiaji.


“Lakini pia baadhi ya mashirika yanasema Watanzania wanaogopwa kwa fujo zao hasa wanapogundua kuwa wanarejeshwa nyumbani,” alisema Burhan. Buruhan alisema tathimini zinaonyesha kuwa vijana wengi wazamia katika nchi za kigeni kwa sababu ya kukosa ajira hapa nchini.


Alisema dalili zinaonyesha kuwa katika miaka ijayo hali itakuwa ngumu zaidi kwa wazamiaji kupata hifadhi au kupokelewa katika nchi nyingine kufuatiwa vitendo vya fujo vinavyofanywa na baadhi yao.


“Tabia za wazamiaji za kuwalazimisha wamiliki wa meli kuwapa fedha kati ya dola US $ 500 hadi 2000 ili wakubali kushuka melini na kupanda ndege bila usumbufu zinawakera sana wenye meli,” alisisitiza.
Alisema maisha ya wazamiaji kwa sasa yako hatarini kufuatia usumbufu wanaowafanyia wamiliki meli, zinazoamua kuwasafirisha kuja nchini.


. Aliwataka vijana wanaojihusisha na vitendo vya kuzamia meli na kwenda katika nchi nyingine, kuacha mara moja ili kuepua kuhatarisha maisha yao.

0 comments

Post a Comment