Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Waziri wa Katiba na Sheria, Celina Kombani: Sitegemei kufukuzwa kazi

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
SIKU moja baada ya CUF, kumshauri Rais Jakaya Kikwete amfukuze kazi Waziri wa Katiba na Sheria, Celina Kombani kwa madai ya kutoa kauli inayowachanganya wananchi kuhusu Katiba, Waziri huyo ameibuka na kusema "Sifikirii kujiuzulu, wala sitegemei kufukuzwa" 
Juzi CUF kilimshauri rais Kikwete kuwapumzisha Waziri Kombani na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema kwa kile ilichoeleza kuwa wamekuwa wakiropoka kuhusu suala la Katiba 
na kuwachanganya wananchi.

Wakati mjadala wa Katiba ukiwa umepamba moto, Waziri Kombani ambaye ndiye waziri mwenye dhamana alisema, "Katiba mpya kwa sasa haiwezekani kabisa kwani sio muhimu na kuwa Serikali haina bajeti ya kushughulikia katiba mpya".

Waziri huyo aliyepewa dhamana ya kuongoza wizara hiyo kwa mara ya kwanza, alisema Serikali itaendelea kufanya marekebisho ya sheria hiyo mama wakati wowote inapolazimika.

“Wachache waje na kitu chenye mashiko na katika maandishi, wakionyesha ni vifungu gani vyenye upungufu, kwa nini vina upungufu na wapendeekeze mbadala wake. Serikali haiwezi kufanyia kazi vitu muhimu kama hivi kwa kupata taarifa kupitia magazetini tu,” alisema Kombani.

Naye Mwanasheria Mkuu wa Seriakali, Jaji Frederick Werema alisema, "Kuandika Katiba mpya hapana, lakini kufanya marekebisho kwa kuondoa au kuongeza mambo fulani kwenye katiba, ruksa.”   Jaji Werema alisema hayo Desemba 27 mwaka jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Ikulu jijini Dar es Salaam baada ya kumalizika kwa hafla ya kumwapisha Jaji Mkuu Mpya, Jaji Mohamed Othman Chande.

 "Suala la kubadilisha ibara zinazoonekana kutokidhi haja na kuingiza mambo mapya kwenye katiba, linakubalika na kwamba hayo yamekuwa yakifanyika," alisisitiza Jaji Werema na kutolea mfano mabadiliko ya katiba yaliyoruhusu kuingizwa kwa haki za binadamu.   Lakini alipotakiwa kuzungumzia kauli hiyo ya CUF jana, Waziri Kombani alisema  hafikirii kujiuzulu wala hajui kama atafukuzwa.   “Mimi sijui kitu.

Nimesema sijui chochote na wala sifikirii kujiuzulu hata suala la kufukuzwa silielewi,”alisema Waziri Kombani.   Wakati Waziri Kombani akisema hivyo, Jaji Werema jana aliliambia gazeti hili kuwa "Sitaki usumbufu, mimi niko likizoni."  Aliendelea ‘Sitaki usumbufu wowote kuhusu hilo na sitaki kusikia habari hizo kabisaaaa.”
Lakini Mwanasheria Mkuu huyo wa Serikali aliwahi kuliambia gazeti hili kuwa hawezi kujiuzulu kwa kauli alizotoa kuhusu Katiba na Dowans.

 "Sijiuzulu ng'o," alisema Jaji na Werema na kuongeza: ''Wanaotaka nijiuzulu ni wale wasiofikiria, kwani kila mtu ana nafasi yake ya kuongea kuhusu katiba. Mimi nimetoa mawazo yangu na wengine wakitaka watoe ya kwao."
Aliendelea, ''Kunitaka nijiuzulu ni fikra za kichanga sana na potofu. Mtu mwenye upeo mpana hawezi kusema Mwanasheria Mkuu ajiuzulu kwa hili,"alisema.

 Juzi, CUF iliitisha mkutano na waandishi wa habari na kueleza kuwa kauli hizo watendaji wakuu wa Serikali kuhusu katiba zinawachanganya wananchi hivyo Rais anapaswa kuwafukuza kazi kwa maslahi ya Serikali yake.

 "Kama Rais Kikwete atakuwa makini, anapaswa sasa kuwapumzisha Kombani na Werema ili wasiendelee kutia doa jeusi Serikali yake ambayo tayari imejaa kila aina ya matatizo," alisema Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
Tags:

0 comments

Post a Comment