Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Arusha: Chatanda adaiwa kuzusha balaa jingine

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
MBUNGE wa Viti maalumu kupitia Mkoa wa Tanga, Mary Chatanda, amezusha balaa jingine baada ya wawakilishi wa madiwani na wabunge wa Chadema, kuamua kususia kikao cha Jumuiya ya Serikali za Mitaa (Alat) kwa kutoa nje.

Chatanda ambaye pia ni Katibu wa CCM mkoani Arusha, anadaiwa kuwa chanzo cha vurugu zilizosababisha mauaji ya waandamanaji waliokuwa wanapinga uchaguzi uliomweka madarakani Meya wa Jiji la Arusha.

Madiwani, wabunge wa Chadema akiwemo mwenyekiti wa Halmashauri ya Karatu, walipinga vikali kwamba Chatanda sio mjumbe wa kikao cha Alat kwa sababu, ubunge wake hautokani na Mkoa wa Arusha.

Tukio hilo lilitokea jana saa 5:00 asubuhi kwenye kikao kilichofanyika jengo la Mkuu wa Wilaya ya Arusha, wawakilishi sita Chadema waliamua kususia kikao hicho kilicholenga kuwachagua wawakilishi wa Alat Mkoa wa Arusha.

Viongozi wa Chadema kwenye kikao hicho waliosusa ni Mbunge wa Jimbo la Arusha mjini, Godbless Lema, Mbunge wa Karatu, Mchungaji Israel Natse, Diwani wa Viti maalumu wilayani Karatu, Cecilia Pareso na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, Lazaro Massay.

Tukio hilo lilianza pale Mbunge wa Jimbo la Karatu, Natse aliposimama na kueleza ya kuwa Chatanda sio mjumbe halali wa kikao hicho kwa sababu, anatoka nje ya Mkoa wa Arusha, hoja hiyo ilipingwa vikali na Diwani wa Terat, Julius Sekeyan.

Wakati hali ya malumbano ikiendelea, Natse alisimamia msimamo wake huku akidai ya kuwa, wanaotakiwa kuwepo ndani ya kikao hicho ni  wenyeviti wa halmashauri wa wilaya ndani ya Mkoa wa Arusha, wakurugenzi wa wilaya, wajumbe wawili wa kuchaguliwa na mabaraza husika na wabunge wa Mkoa wa Arusha.

"Mary Chatanda sio mjumbe halali katika kikao hiki, huyu anatoka Tanga sasa iweje leo tufanye uchaguzi wa viongozi wa Alat Mkoa wa Arusha, awe mpiga kura kwanini asiende kusubiri uchaguzi wa Tanga?" alihoji Natse

Wakati hayo yakiendelea, Chatanda alikuwa amekaa kwenye kiti chake, huku akionekana usoni mwake kama mwenye jazba na muda wote alikuwa akichezea simu yake ya mkononi.

Hata hivyo, viongozi wa muda ndani ya kikao hicho, akiwemo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Arusha Vijijini, Halifa Hidda, waliamua kutoa ufafanuzi na kwamba, hata Chadema wakisusia wao wataendelea na uchaguzi kama kawaida.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti baada ya kutoka ndani ya ukumbi huo, baadhi ya wawakilishi wa Chadema wakiongozwa na Mchungaji Natse, walidai uamuzi wa kususia kikao hicho ulitokana na madai ya kupinga kitendo cha Chatanda kuwepo ndani.


Sent from my iPhone
Tags:

0 comments

Post a Comment