Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Majangili waua faru wa JK

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter FARU mmoja kati ya watano waliopokewa na Rais Jakaya Kikwete kutoka nchini Afrika Kusini na kuingizwa kwenye mbuga ya wanyama ya Sengereti, ameuawa na majangili ambao wametoweka na pembe zake.

Faru huyo dume aliyekuwa akijulikana kwa jina la George (12), aliletwa nchini na kampuni ya uwekezaji ya Grumeti Reserve na Kikwete aliahidi kuwa wanyama hao watapewa ulinzi mkali kuliko ule anaopewa yeye.

Lakini habari zilizolifikia gazeti hili na kuthibitishwa na kaimu mkurugenzi mkuu wa Shirika la Hifadhi Tanzania (Tanapa), Edward Kishe zinaeleza kuwa faru huyo aliuawa Desemba 12 mwaka huu na kukatwa pewmbe zake.
Inaaminika kwenye baadhi ya jamii, hasa Mashariki ya Kati na ya Mbali, kuwa unga unaotokana na pembe za faru, ambao ni kati ya wanyama walio hatarini kutoweka, una chembechembe ambazo zina dawa yenye nguvu sana na hivyo kufanya majangili wawasake wanyama hao kwa jitihada kubwa.

Kabla ya kukutana na waandishi iliwalazimu kukaa kikao kati ya uongozi wa Frankfurt Zoloogical Society, Grumeti Reserve na Tanapa kuanzia saa 9:00 alasiri hadi saa 12:00 jioni.

Akiongea na waandishi wa habari, Kishe alisema: ”Ni kweli faru huyo aliuawa Desemba 12 na mzoga wake ukapatikana Desemba 14 mwaka huu ukiwa hauna vipusa.”
Alisema kabla ya hapo kifaa cha mawasiliano ambacho faru huyo na wenzake wanne waliwekewa, kilipoteza mawasiliano na walinzi na katika kufuatilia walibaini kuwa faru huyo aliuawa na majangili katika eneo Nyabeho lililoko karibu na vijiji vya Ikoma na Robanda.

Alikiri kukithiri kwa ujangili na kuwa matukio ya uwindaji wa tembo yanachukua nafasi kubwa katika hifadhi hiyo na nyingine na hali hiyo inalifanya shirika kuongeza watu na vifaa.

Alipotakiwa kutoa ufafanuzi kama tukio hilo halitakuwa limewavunja moyo na kuharibu mahusiano na wadau waliosaidia ,alikataa na kudai hata huko Afrika Kusini matukio kama hayo yamekuwa yakitokea.
Kuhusu ahadi ya kuwawekea faru hao ulinzi mkali unaozidi wa rais, mhifadhi mkuu wa Serengeti, Mtango Mtahiko alisema tukio hilo limewastua sana kwa kuwa wanafanya jitihada kubwa za kuwalinda faru, ambao ni aina moja kati ya tano za wanyama wakubwa barani Afrika ambao ni kivutio kikubswa cha utalii.

Alisema wanajitahidi kuongeza nguvu kwenye ulinzi ili kukabiliana na matukio hayo. Kuanzia mwishoni mwa mwaka 2009 hadi sasa, zaidi ya tembo 15 wameuawa na meno kuchukuliwa.

Hata hivyo alisema hawajajua soko kuu la meno ya tembo liko wapi ,hata hivyo alikiri kuwa kuna taarifa za kuwepo kwa soko zuri la meno ya tembo na kuwa wanashirikiana na polisi kwa upelelezi.
Mei 21 mwaka huu Faru watano ambao ni Cleo (ke), Ethna (ke), Lunnar (ke), Benj (me) na George (me) ambaye ameuawa.
Akipokea faru hao, Rais Kikwete alisema Afrika Kusini imeongeza uwezo kwa Tanzania kwa kuleta faru hao weusi na kuwa ongezeko hilo ni la manufaa kwa taifa na kuahidi kuwa "huduma zake na ulinzi zitakuwa za kipekee zaidi yangu mimi”.
Naye waziri wa zamani wa Maliasili na Utalii, Shamsa Mwangunga alisema kwa miaka 1970-1980 ujangili ulipunguza faru na kwamba "sasa tutahakikisha hakuna ujangili kwa faru... tutaweka askari maalum wa kuwalinda wanyama hao”.
Mkurugenzi wa Sangita Grumeti, Brian Harris alisema faru hao walitolewa kwenye zuu na kuwa kazi zote ikiwa ni pamoja na kununua na kuwasafirisha ziligharimu Sh7.5 bilioni.

Mmoja kati ya Faru watano waliotoka nchini Afrika Kusini na kuingizwa kwenye mbuga ya wanyama ya Sengereti.



Mkurugenzi wa Frankfurt Zoloogical Society, Gerard Bigurube ambaye awali alikuwa mkurugenzi mkuu wa Tanapa, alisema wajibu wao ni kuwezesha usafiri, mafunzo kwa askari na kuhakikisha hakuna madhara kwa wanyama hao.
Habari zaidi zinasema kuwa maslahi madogo kwa askari na viongozi kupuuza ushauri wa kuwaweka faru hao kwenye hifadhi ndogo yamechangia kuzorota kwa ulinzi wa wanyama hao.

Habari zinasema askari wachache wa hifadhi hulazimika kufanya doria mchana na usiku ili kukabiliana na wimbi kubwa la majangili wanaotumia silaha mbalimbali, zikiwemo za kivita.

Uchunguzi wa kina uliofanywa na gazeti hili ulibaini kuwa mara baada ya kuletwa faru hao askari wadogo walishauri wawekwe kwenye zuu lakini
uongozi wa hifadhi uliwapuuza na kudai wangeimarisha doria kwa kuwa walifungiwa vifaa maalum vya mawasiliano.
Baadhi ya askari ambao hawakutaka majina yao yaandikwe walisema kasi ya ujangili haitaweza kupungua kutokana na mianya ya kiutendaji
iliyopo ndani ya hifadhi hiyo ,likiwemo suala la maslahi duni.

Walisema askari  hulipwa tsh,10,000=wawapo doria bila kuangalia ni wakati wa operesheni kama ilivyo wakati huu ambao inadaiwa pori hilo limevamiwa na majangili wenye silaha za kivita.

Alipoulizwa kuhusu suala hilo, kaimu mkurugenzi mkuu wa Tanapa, Edward Kishe  alikana na kudai kuwa wanajitahidi kuwatimizia maslahi yao, lakini hakubainisha kama wameyaboresha kwa kiasi gani.

Akiongea na Mwananchi kwa njia ya simu mara baada ya kuapishwa, Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige kuwepo matatizo kwenye wizara  na kuahidi kufanya mabadiliko makubwa ili kuiboresha.
Tags:

0 comments

Post a Comment