Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - HABARI ZA LEO - Bunge halina uwezo kutunga Katiba mpya

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
MWANASHERIA Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Othman Masoud amesema Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania halina uwezo wa kutunga Katiba mpya, bali kuifanyia marekebisho iliyopo."Bunge la Jamhuri halina uwezo wa kutunga Sheria ya Katiba hili ni jambo la msingi sidhani Zanzibar na watu wake kama watakubali kuvunja Katiba," alisema.

Masoud alisema hayo jana akitoa mchango wake katika mjadala wa maoni ya Muswada wa Sheria wa Mapitio ya Katiba unaoendeshwa na Kamati ya Bunge, Sheria na Katiba ya Bunge la Muungano
uliofanyika katika Hoteli ya Bwawani mjini hapa.

Alisema msingi wa hoja yake unatokana na Kifungu cha 98(1)(b) cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano kinachoeleza. Kifungu hicho kinasema: "Muswada wa Sheria kwa ajili ya kubadilisha masharti yoyote ya Katiba hii au masharti yoyote ya Sheria yoyote yanayohusika na jambo lolote kati ya mambo yaliyotajwa katika Orodha ya Pili kwenye Nyongeza ya Pili iliyoko mwishoni wa Katiba hii, utapitishwa tu iwapo utaungwa mkono kwa kura za Wabunge ambao idadi yao haipungui theluthi mbili ya Wabunge wote kutoka Tanzania Bara na theluthi mbili ya Wabunge wote kutoka Tanzania Zanzibar."

Orodha hiyo ya pili kwenye nyongeza ya pili iliyoko mwishoni wa Katiba inaeleza mambo ambayo mabadiliko yake yanahitaji kuungwa mkono na theluthi mbili ya wabunge wote kutoka Tanzania bara na theluthi mbili ya wabunge wote kutoka Tanzania visiwani moja likiwa mambo ya muungano ambalo suala la Katiba ni mojawapo.

Alisema Bunge lililopo sasa haliwezi kutunga Katiba mpya, bali kazi yake ni kurekebisha hivyo linatakiwa liwepo Bunge jingine ambalo litakuwa maalumu kwa ajili ya kutunga Katiba.

Akiwasilisha madhumuni na sababu za muswada huo, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta alisema umependekeza kutungwa kwa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya nchi ya mwaka 2011 na unakusudia kuanzishwa kuweka masharti ya uanzishaji wa tume pamoja na sekretari kwa madhumuni ya kuendesha na kusimamia mchakato wa mabadiliko ya hayo.

Mchakato wa mabadiliko ya Katiba pamoja na mambo mengine, utaangalia chimbuko na uhusiano wa katiba iliyopo kwa kuzingatia uhuru wa wananchi na mfumo wa siasa.

Alisema pindi muswada huo utakapopitishwa na kuwa sheria, utakuwa na utaratibu wa kisheria utakaomwezesha Rais kuunda tume ya kukusanya maoni kuhusu katiba na kuunda Bunge la Katiba kwa madhumuni ya kutunga Katiba mpya.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Jimbo la Kwamtipura, Hamza Hassan Juma amesema muswada wa marekebisho ya Katiba ya Muungano una upungufu mwingi ukiwemo kutoshirikishwa kwa Serikali ya Zanzibar ambayo alisema haikushirikishwa kikamilifu ili kutoa maoni yake na wala haukupelekwa katika Baraza la Wawakilishi kupata maoni ya Baraza, hivyo haukustahiki kupelekwa Bungeni kujadiliwa kwani umekosa ridhaa za pande mbili.

“Muswada huo ni vyema kurudi serikalini na ukafanyiwe marekebisho na badala yake upelekwe katika Baraza la Wawakilshi ili upate ridhaa ya nchi mbili zilizoungana,” alisema Hamza.

Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Dk. Omar Dadi Shajak alisema kwa kuwa utaratibu haukufuatwa basi muswada huo haufai.“Taratibu hazikufuatwa na misingi ya kujadili kama Jamhuri ya Muungano mchakato wa muswada huu haukubaliki kwani utaratibu haukufuatwa,” alisema Shajak.

Alisema mu8swada huo uko upande mmoja na umepitishiwa bungeni bila kuzingatia pande mbili zilizounda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jambo ambalo haliwezi kuachiwa kupita hivyo hivyo kwani kufanya hivyo ni kuidharau Zanzibar ambayo ni mshirika kamili katika Muungano huo.

“Muswada huu wote urejeshwe bungeni na utengenezwe tena kama kwa kuweka usawa au vyinginevyo, lakini kwa hivi haukubaliki kabisa,” alisema Shajak.

Shajak alisema katika Bunge, jambo linalohusu Katiba ya Zanzibar na suala lolote lile la Muungano ni vyema kutumika usawa wa wajumbe Zanzibar na Bara na siyo kuamuliwa tu na wajumbe kutoka upande wa Tanzania bara peke yao.Mjumbe kutoka CCM, Ali Mwinyi Msuko aliwataka wanasheria wa Zanzibar kukutana na wenzao wa Tanzania bara kuupitia upya muswada huo akisema hakuna sababu ya kuuharakisha kuufikisha bungeni.

Waziri wa Kilimo, Mansour Yusuf Himid alisema muswada huo una lengo la kuwadanganya Wazanzibari na hakuna jambo jingine.“Nashukuru siku hii ya leo, Kamati ya Bunge imekuja kutudanganya Wazanzibari na siku ya leo nina huzuni kubwa sana kama Mtanzania, kama Mzanzibari, naona kiini macho tu tunafanyiwa kama Baraza la Wawakilishi hawajashirikishwa, basi hakuna haja ya kukubali hilo,” alisema kuongeza:

“Lazima tushirikishwe ipasavyo. Tumeungana kwa hiari. Hii ni Jamhuri ya pande mbili tumekwenda kwa hiari, tutarudi kwa hiari, tutabaki kwa hiari. Kama Wazanzibari hawajashirikishwa kupitia kura ya maoni na kufanyiwa kiini macho hicho, basi wasikubali kudanganywa," alisema huku akiungwa mkono na wananchi wengine walioshiriki mjadala huo.

Mansoor ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Kiembesamaki (CCM), alisema binafsi anaupinga muswada huo huku akisema hiyo ni nafasi pekee ya kuhakikisha muungano unafanyiwa marekebisho na kwamba hiyo ni fursa ya pekee kwa wananchi wa Zanzibar kupinga kwani hawataipata tena iwapo muswada huo utapita.

“Hii ndiyo fursa yetu ya mwisho Wazanzibari, nikwamabie tukicheza hapa ndiyo basi hatutakiona kitu chochote ndiyo basi tena,” alisisitiza.Mwandishi wa habari mwandamizi wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), Ally Saleh alisema muswada huo haukugusia Katiba ya Zanzibar jambo alillotafsiri kama dharau juu ya makubaliano ya Muungano.

“Kura ya maoni ni kitu gani? Je, Wazanzibari wakisema hawataki athari yake itakuwa nini? Tusifikiri Wazanzibari watapinga Katiba je, athari zake zitakuwa ni nini? Kusema tume isipelekwe mahakamani huko ni kuizuia demokrasia,” alisema.

0 comments

Post a Comment