Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - HOJA YA KATIBA:JK amvuruga Mnyika

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
KAULI ya Rais Jakaya Kikwete kwamba anaanza mchakato wa kuandikwa upya Katiba ya Tanzania, imefilisi hoja binafsi ya Mbunge wa Ubungo, John Mnyika  ambaye jana alitoa tamko rasmi kueleza kuwa amesitisha kwa muda mpango wa kuiwasilisha hoja hiyo bungeni, mwezi Februari mwaka huu.

Katika tamko hilo lenye kurasa sita na kichwa cha habari "Kauli yangu juu ya tamko la Rais Kikwete kuhusu Katiba Mpya" Mnyika alisema kwa mazingira yaliyopo, anasubiri utekelezaji wa serikali katika suala hilo.

"...Katika mazingira hayo, nasubiri kwanza ufafanuzi wa serikali kuhusu mchakato huu ikiwemo kujua kwa kina muundo wa tume, hadidu za rejea na kama serikali itapeleka bungeni mapendekezo kuhusu mchakato, kabla ya kutoa kauli kuhusu hatma ya hoja binafsi ambayo nilitoa taarifa kuwa nitaiwasilisha bungeni katika mkutano wa mwezi Februari,"alisema Mnyika na kuendelea:

"na katika kipindi ambacho nasubiri ufafanuzi wa serikali ambao inapaswa kuuweka hadharani, nitaendelea na hatua ambazo nilizitangaza nilipokwenda kuwasilisha taarifa ya hoja tarehe 27 Desemba 2010.

"

Mnyika ameendelea kueleza katika tamko hilo kuwa " kutokana na kauli ya Rais Kikwete na hatua za ziada ambazo natarajia kutoka kwa serikali, nitatumia wiki ya kwanza ya mwezi Januari kukutana ana kwa ana na baadhi ya viongozi wa asasi za kiraia, taasisi za dini na vyama vya siasa ikiwemo Chadema, kuweza kushauriana hatua za ziada za kuchukua."

Aidha alisema "natambua kuwa kauli ya Rais Kikwete kukubali kuandikwa kwa katiba mpya, inaashiria mabadiliko ya kimtazamo kwa upande wake pia ukilinganisha na kauli zake mbalimbali katika kipindi cha kuanzia mwaka 2005 mpaka mwaka 2010 kuhusu suala la mabadiliko ya mfumo wa utawala katika taifa, hali inayoashiria kwamba ametambua kuwa umuhimu wa katiba mpya ni wa Watanzania waliowengi."

Hata hivyo alieleza kuwa pamoja na rais kukubali kuandikwa kwa katiba mpya, bado Watanzania wanahitaji kujadili kwa kina na kwa haraka kuhusu mchakato uliopendekezwa ili taifa liende katika mkondo sahihi wa kuanza kutoa maoni.

"Suala hili ni la msingi kwa kuwa Historia ya Taifa letu inaonyesha kwamba Tume zilizoundwa na Marais na kushughulika na masuala yanayogusa Katiba hazikuweza kukidhi matakwa ya wananchi kwa sababu mbalimbali," alisema Mnyika na kuongeza:

"Mathalani, taifa linajadili sasa kuhusu mabadiliko ya katiba kutokana na kasoro katika hatua za awali za kuandikwa kwa Katiba ya Kudumu ya Tanzania ya mwaka 1977 ambayo ndiyo tunayoitumia hivi sasa pamoja na marekebisho yake."

Aliendelea "Mchakato uliotumiwa na Rais wa wakati huo, Marehemu  Julius Nyerere ndio ambao unajitokeza sasa kwenye hotuba ya Rais Kikwete kwa kueleza kwamba Rais anaunda tume na baadaye mapendekezo ya tume yanakwenda moja kwa moja kwenye vyombo vya kikatiba bila kwanza kuwa na matokeo ya utaratibu huu, ni wananchi kutoshirikishwa kwa ukamilifu wake katika maamuzi yanayohusu katiba."

"Matokeo ya mfumo huo ni kuandikwa kwa katiba isiyokubalika na umma kwa uwingi wake na kusababisha mpaka sasa marekebisho (viraka) mara kumi na nne na bado kuna mapungufu mengi kwa kiwango cha sasa kukubaliana kuandika katiba mpya," alisema.

"Katika mazingira hayo, ndipo panapojitokeza umuhimu wa kuwa na Mkutano Mkuu wa Taifa  wa katiba kabla ya mapendekezo ya katiba kupelekwa kwenye mamlaka za kikatiba ambazo kwa mujibu wa katiba ya sasa ibara ya 98 ni Bunge pekee."

Mnyika aliendelea kueleza kuwa kauli ya Rais Kikwete inaashiria kwamba wananchi hawatahusishwa moja kwa moja kwenye kuamua katiba, badala yake tume itachukua maoni yake na baadaye maamuzi yatafanywa na bunge kwa niaba yao kama ilivyo kwenye marekebisho ya kawaida ya katiba kwa mujibu wa ibara ya 98 ya katiba.

Mbunge huyo kwa tiketi ya Chadema, aliwasilisha taarifa ya kutaka kupeleka bungeni hoja binafsi ya Katiba Mpya Desemba 19 mwaka huu ambapo pamoja na mambo mengine alipinga pendekezo la Waziri Mkuu Mizengo Pinda la kuunda tume ya kuangalia mchakato huo.

"Ibara ya 8 kifungu cha kwanza cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na mapungufu yake inaeleza wazi umuhimu wa wananchi kushirikishwa katika uundwaji wa katiba. Pia Ibara ya 63-(2) nayo inaeleza wazi," alisema Mnyika.


Aliongeza kuwa kama mbunge ana haki ya kuwasilisha hoja binafsi kuhusu katiba mpya na kwamba ni vyema suala la uundwaji wa katiba likarejeshwa mikononi mwa Bunge kwa kuwa ni mhimili wa dola unaofanya kazi kwa niaba ya wananchi.

"Ibara ya 98 ya katiba ndio sehemu  pekee inayozungumzia marekebisho ya katiba hivyo ni wakati muafaka suala hili la katiba likapelekwa bungeni ili wananchi wawakilishwe," alifafanua Mnyika.

"Unajua katiba ni sheria na kwa kuwa bungeni ndiko kunakotungwa sheria basi wanaopaswa kutoa mwelekeo wa katiba mpya ni Bunge," aliongeza.

"Pia katiba ni mkataba kati ya wananchi na watawala... ikumbukwe kuwa anayeandika mkataba ni mwenye mali, na hapa mwenye mali ni mwananchi na Bunge lipo kwa ajili ya wananchi. Kutokana na hilo, ipo kila sababu ya suala hili kurudi bungeni."

Msimamo wa Mnyika kupeleka hoja binafsi bungeni aliutoa siku mbili baada ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuamua kulibeba suala la madai ya katiba mpya, akisema kuwa atamshauri Rais Jakaya Kikwete kuunda timu ya kushughulikia suala hilo.

Pinda alitangaza uamuzi huo Desemba 19 katika mkutano na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam katika kipindi ambacho kilio cha katiba mpya kinaongezeka kila kukicha.

“Isije watu wakadhani serikali ina kigugumizi; hapana. Sasa mjadala umeiva na ni vizuri lizungumzwe kwa utaratibu. Nipo tayari kuzungumza na rais. Nitamshauri mzee (rais) na nitaweka nguvu zangu huko, hilo halitawezekana tusipoweka ‘initiative’ (juhudi),” alisema Pinda.

"Watu wasifikiri wala kuona kuwa serikali haioni kama madai ya katiba mpya kuwa si ya msingi.
“La pili, tunataka kuzungumza machache, lakini kubwa ni hili la katiba mpya. Kumekuwa na maelezo mengi, marefu, mjadala mkali;

sasa hili nataka niseme tusione kama madai ya katiba si ya msingi sana; hapana. Ni ya msingi. Kwa serikali mabadiliko ya katiba ni utaratibu wa kawaida kwani ni jambo lililo ndani ya katiba,” alisema Pinda.

“’All along’  Watanzania wameendelea kuibuka na kudai tume huru ya uchaguzi na katiba mpya. Tulipofikia tunaulizana 'kuna ugumu gani kukaa na kuandika katiba mpya?"

Aliongeza kusema: "Mimi binafsi sioni tatizo kwa hilo kufanyika, lakini kama serikali zipo namna mbili za kulishughulikia. Moja ni kutafuta utaratibu wa kumshauri rais aunde kamati ya watu wangalie maeneo gani ya kuingiza katika katiba hata ikibidi wananchi waulizwe yatoke ya kuwekwa mezani kwa kuhusisha vyama vya siasa na wanazuoni.”

Pinda aliitaja njia ya pili kuwa ni rais kuunda timu yake ya kiserikali itakayoangalia mapendekezo ya tume zilizoundwa awalikuangalia marekebisho ya katiba na kuchukua mapendekezo yaliyojirudia yatakayoonekana kufaa kuingia katika katiba.

Alisema kutokana na tume hizo yapo yaliyotekelezwa na yale ambayo yaliahirishwa akisema kuwa pengine ni kutokana na wakati. Hata hivyo alisema ni bora kuruhusu tume itakayokuwa pana na kuyatazama mapendekezo ya tume za awali, kuangalia na kushauri akisema kuwa huenda ikaona mambo mengine.

“Ni bora kuruhusu tume pana ya kutazama, tushauri na kuangalia, pengine tukiyaona ya utawala si katiba mpya bali kitu kingine. Katika katiba yapo mema mengi tusiangalie ubaya tu, katiba hiyo ndiyo imetufikisha hapa taifa likiwa na sifa za utawala bora na mambo mengine,” alisema Pinda.

Lakini Mnyika alipingana na Pinda kuhusu hoja ya kuundwa kwa timu ya kuchunguza madai hayo akisema "Sikubaliani na kauli ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuhusu katiba.”

“(Waziri Mkuu) Amesema atamshauri rais kuunda timu itakayoangalia mapendekezo ya tume zilizoundwa na pia kuanzisha utaratibu wa marekebisho ya katiba. Naona kauli yake haijalenga kuwepo kwa katiba mpya, bali inalenga zaidi marekebisho ya katiba."

Hata hivyo mjadala huo wa katiba ulifungwa Desemba 31 mwaka jana baada ya Rais Jakaya Kikwete kutangaza kuanza mchakato wa kuandikwa kwa Katiba Mpya.

"Nimeamua kuunda tume maalumu ya Katiba, yaani Constitutional Review Commission. Tume hiyo itakayoongozwa na Mwanasheria aliyebobea, itakuwa na wajumbe wanaowakialisha makundi mbalimbali katika jamii yetu kutoka pande zetu mbili za Muungano," alisema Rais Kikwete alipokuwa akitoa salamu zake za mwisho wa mwaka.

Tangu kumalizika uchaguzi mkuu wa Oktoba 31, Chadema imewasha moto wa mabadiliko ya katiba na kufufua mjadala wa kutaka kuandikwa kwa katiba mpya kiasi cha Waziri Pinda kuamua kutoa tamko  kuwa atamshauri Rais Jakaya Kikwete aunde tume kuchunguza madai hayo.


Miongoni mwa viongozi waliojiunga kwenye mjadala huo wa kutaka katiba mpya ni mawaziri wakuu wa zamani, Joseph Sinde Warioba na Frederick Sumaye, Jaji Mkuu Agustino Ramadhan na Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa ambaye alitahadharisha kuwa bila ya katiba mpya nchi inaweza kuingia kwenye vurugu.
Tags:

0 comments

Post a Comment