Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Dawa ya Ukimwi yagunduliwa.

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Tanzania, Profesa David Mwakyusa
Leon Bahati
WAKATI wanasayansi waliogundua dawa ya Ukimwi wakiweka bayana jinsi inavyofanya kazi mwili kupambana na ugonjwa huo, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Profesa David Mwakyusa amemshukuru Mungu kwa taarifa za ugunduzi wa dawa hiyo.Taarifa ya kupatikana kwa dawa hiyo zilitangazwa mwishoni mwa wiki na wanasayansi wa Taasisi ya Magonjwa ya Kuambukiza na Mzio (Niaida) ya Marekani, akisema kuwa tiba hiyo inaweza kutibu ugonjwa huo hatari kwa asilimia 90, kiwango kinachoiweka dawa hiyo kwenye uwezekano mkubwa wa kupitishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) na hivyo kuanza kutumika rasmi.

Dawa hiyo huchochea mwili na kuuongoza katika kujitengenezea aina ya chembechembe za kinga zenye uwezo wa kukabili virusi vya ukimwi. Chembechembe hizo zimepewa jina la kitaalamu la VRCO1 na VRCO2 ambazo utafiti wake umeonyesha kuwa zinaweza kuvikabili virusi vya Ukimwi kwa asilimia 90.

Habari hizo, ambazo zimekuwa gumzo duniani kote, zilimfurahisha pia Waziri Mwakyusa, wakati wasomaji wa Mwananchi walikuwa wakituma maoni yao kuzungumzia matokeo ya utafiti wa dawa hiyo, wengi wakifurahia kuwa sasa "wamewekwa huru".

Akizungumza na Mwananchi, Prof Mwakyusa alisema: "Serikali imekuwa ikifanya juhudi mbalimbali katika kuhakikisha kwamba wananchi wake wanapata huduma za tiba hata kama ni ghali kiasi gani.

"Kama ni kweli dawa hiyo imepatikana, ni jambo la kumshukuru Mungu kwa kuwa Ukimwi ni ugonjwa ambao umeiathiri sana dunia."

Alisema serikali imekuwa ikitumia mamilioni ya fedha kupambana na ugonjwa huo na hivyo kuwezesha dawa nyingi ghali duniani zinazopunguza makali ya ugonjwa huo na kutibu magonjwa sugu kutolewa bure kwa wananchi.

Alitoa mfano wa dawa hizo kuwa ni zile za kutibu malaria maarufu kwa jina la Alu, dawa za kutibu kifua kikuu na zile za kupunguza makali ya ukimwi.

"Na hata kama hizo za kutibu ukimwi zitakuwa zimepatikana, bado mataifa makubwa yana wajibu wa kuhakikisha zinaweza kuwafikia kirahisi watu katika nchi masikini," alisema Profesa Mwakyusa.

Kwenye chumba cha habari cha Mwananchi, wasomaji walikuwa wakipiga simu kuelezea kufurahishwa na taarifa hiyo huku wengine wakitoa maoni yao kwenye mtandao, wengi wakisifu matokeo ya utafiti huo na wengine wakisema kuwa bado kuna safari ndefu.

Nchini Marekani, wanasayansi wa Niaida waliweka bayana namna dawa hiyo inavyoweza kufanya kazi katika mwili wa binadamu wakati wa kupambana na ugonjwa huo hatari.

Niaida imetoa taarifa hiyo kufuatia taarifa iliyotangazwa wiki iliyopita kwamba wamegundua chembechembe za kinga ambazo zinaweza kutumika kutibu ugonjwa wa ukimwi kwa asilimia 90.

Mkurugenzi wa Niaida, Dk Anthony Fauci alisema katika taarifa kwenye mtandao wa taasisi hiyo kwamba dawa waliyoigundua siyo ya kwenda kuua moja kwa moja virusi vya Ukimwi kwenye mwili wa binadamu, bali ni kuchochea mwili na kuuongoza katika kujitengenezea aina ya chembechembe za kinga zenye uwezo wa kukabili virusi vya ukimwi.

Dk Fauci alisema kuwa chembechembe hizo, VRCO1 na VRCO2, zinapambana tu na virusi vya Ukimwi jambo ambalo linawapa faraja kuwa chembechembe hizo haziwezi kusababisha madhara kwa mwili wa binadamu.

Mtaalamu huyo alieleza kwamba kinachofanywa na chembechembe za kinga za VRCO1 na VRCO2 kwenye mwilini binadamu, ni kuvibana virusi vya Ukimwi na kuvifanya vishindwe kuendelea kushambulia seli nyeupe za damu.

Kwa kawaida virusi vya Ukimwi hushambulia seli nyeupe za damu ambazo ni muhimu katika kusaidia mwili kujikinga na maradhi ama kwa jina jingine la kitaalamu CD4, ambako virusi vya Ukimwi hugeuza kuwa makazi yake.

Kila seli nyeupe inayoshambuliwa, wataalamu wanasema, hufa baada ya kutumika kuzalisha virusi wengine na mzunguko huo huendelea hadi mwili unapojikuta umepungukiwa na kinga kiasi cha kushindwa kuhimili vishindo vya maradhi ya kawaida.

Wataalamu wanasema hali hiyo ndiyo inayomfanya mwathirika wa Ukimwi kufa.

Dk Fauci alisema Chembechembe za  VRCO1 na VRCO2 hubana mashambulizi ya virusi vya Ukimwi kiasi cha kushindwa kuendelea na uharibifu wa CD4.

Kwa sababu hiyo, alisema dawa watakayoitoa katika hatua ya kwanza kupitia chanjo ni kwa ajili ya kuufundisha mwili namna ya kutengeneza chembechembe za VRCO1 na VRCO2 ambazo zitakabiliana na virusi wa ukimwi.

"Kwa kutumia teknolojia tuliyogundua tutatengeneza aina ya chanjo ambayo kazi yake itakuwa ni kuufundisha mwili namna ya kutengeneza chembechembe za kinga aina ya VRCO1 ambazo zitakuwa na uwezo wa kupambana na virusi vya ukimwi," alisema Dk Fauci.

Wanasayansi wa Niaida walioshiriki kwenye utafiti huo ni Dk Peter Kwong, Dk John Mascola na Dk Gary Nabel.

Wataalamu hao wanaelezewa kuwa waliongoza timu mbili ambazo ziliendesha utafiti huo ambao ulihusisha damu za waathirika kutoka karibu kona zote za dunia.

“Tulitumia utaalamu wetu kujenga mazingira yote ya virusi wa Ukimwi na ndio tukaweza kufahamu namna ya kujenga mazingira ya kudhibiti virusi hivyo," alisema mmoja wa wajumbe wa jopo la madaktari hao waandamizi, Dk Nabel.

Aliongeza: "Haikuwa kazi rahisi kwa sababu virusi vya Ukimwi vina tabia ya kujibadilishabadilisha. Na hii ndiyo imekuwa ikiwapa taabu wataalamu wengi katika kupata tiba.

"Kujibadilishabadilisha huko kumefanya dunia kuwa na aina mbalimbali za virusi. Utafiti wetu umewezesha kutengeneza mazingira ya kukabiliana na namna zote za virusi kuweza kujigeuzageuza."

Isitoshe Dk Nabel alisema chembechembe za kinga za VRC01 na VCR02 zina uwezo wa kupenya mazingira yote ambayo CD4 za mwili zinaweza kupatikana.

Dr Mascola yeye alielezea ufanyakazi wa VCR01 na VCR02 kuwa ni wa ajabu kwa sababu zinapambana na aina zote za utendaji wa virusi vya Ukimwi.

Wataalamu hao walisema VRC01 na VRC02 haviingilii itendaji kazi wa seli kwa namna yoyote ile bali kukabiliana na harakati za virusi vya ukimwi.
Dk Faci alisema haya ni maendeleo mazuri katika kipindi hiki ambacho waathirika wa Ukimwi wamekuwa wakitumia tu dawa za kutuliza makali ya virusi.

Maelezo ya wataalamu ni kwamba anayetumia dawa za kupunguza makali ya virusi vya Ukimwi atatumia maisha yake yote na huwa hazitibu.
Lakini katika ugunduzi wa dawa yao, Dk Fauci alisema binadamu atapatiwa chanjo hiyo kwa mara moja na itatosha kabisa kuuweka mwili wake katika kuandaa majeshi ambayo yatakabiliana na virusi.

Tayari baadhi ya wataalamu wamekiri kuwa ugunduzi huo wa Niaida umeleta mapambazuko ya tiba ya ugonjwa huo na mojawapo ni Mamlaka ya Chakula na Dawa Marekani ambayo imesema kuwa dawa hiyo haitakuwa na madhara yoyote kwa binadamu.

Dk fauci amewahi kuongoza Taasisi ya Taifa ya Afya (NIH) ya Marekani kuanzia mwaka 1968 na kuaniza 1974 aliteuliwa kuongoza vitengo mbalimbali maalumu vya tiba nchini humo.

Aliteuliwa kuwa mkuu wa kitengo cha utafiti wa tiba cha Niaida mwaka 1980 na mwaka 1984 akateuliwa kuwa mkurugenzi wa taasisi hiyo, nafasi ambayo anaishikilia hadi sasa.
Tags:

0 comments

Post a Comment