Subscribe to receive latest Updates

Online :

You Are Here: Home - - Lipumba adai Kikwete ni tatizo la mpasuko CCM

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter

WAKATI hali ya kisiasa ndani ya CCM ikiwa ni tete, mwenyekiti wa CUF Profesa Ibrahim Lipumba amesema Rais Jakaya Kikwete ndiyo chanzo cha malumbano baina ya wabunge wa chama hicho yanayoendelea sasa.

Wabunge wa CCM na baadhi wanachama wamekuwa katika malumbano makali yanayosababishwa na tuhuma za ufisadi, malumbano ambayo yamesababisha warushiane maneno ya kudhalilishana huku wakianza kuanika vyanzo vya mapato vya chama hicho kwenye chaguzi na shughuli mbalimbali.

Akizungumzia hali hiyo ambayo imejitokeza kwenye mkutano wa kamati iliyounda kutafiti chanzo cha kutoelewana ndani ya CCM, Lipumba aliwaambia waandishi jana kuwa tabia ya Rais Kikwete kutaka kuwa mwema kwa makundi yote hasimu ya chama hicho na kushindwa kutoa msimamo wake kama kiongozi mkuu, ndio chanzo cha tishio hilo la kusambaratika kwa CCM.

Hali mbaya zaidi ilijidhihirisha wiki hii wakati wabunge na mawaziri walipotuhumiana kwa kukumbatia mafisadi huku baadhi wakijitoa muhanga kuwatetea wenzao wanaotuhumiwa kwa ufisadi.

Baadhi wamediriki kumtuhumu waziri mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, mwanasheria mkuu wa zamani, Andrew Chenge na mweka hazina wa zamani wa CCM, Rostam Aziz kuwa ndio vinara wa ufisadi, hoja ambazo zimepingwa kwa madai kuwa wanaonewa na kwamba kuna haja ya kuchunguza upya kashfa ya Richmond. Lakini aliona yote hayo yametokana na udhaifu wa Kikwete.

Akizungumza na Mwananchi muda mfupi baada ya kuwasili nchini akitokea Maputo Msumbiji, ambako alienda kusimamia uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 26, Lipumba alisema Rais Kikwete, ni tatizo.

Profesa Lipumba alituhumu kwamba masuala ya kashfa ya Richmond, uchunguzi wa posho mbili na wizi katika uchaguzi wa 2005, yote yalibarikiwa na Ikulu na kwamba ndio chanzo cha vurugu hizo zinazoyumbisha dola hivi sasa.

“Rais ndiye aliyebariki mkataba wa Richmond kwa sababu yeye ndiye mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri na hakuna mtu yeyote anayeweza kutengua maamuzi ya baraza hilo isipokuwa rais," alisema Lipumba.

"Sasa leo anashindwa kusimamia uwajibishwaji wa wahusika; anajua kila kitu na ushahidi umetolewa wa kutosha.

“Ikulu inajua kuwa mkurugenzi wa Takukuru, Dk Edward Hoseah si msafi na ushahidi umetolewa wa kutosha kwa kuhusika kwake na Richmond, cha kushangaza Waziri Mkuu Mizengo Pinda anasema Ikulu ndiyo iliyomuagiza Hoseaa kuwachunguza wabunge.”

Hata hivyo, Ikulu imekuwa ikitetea kwamba Rais Kikwete hajawahi kubariki mkataba wa Richmond na ni mtu wa kwanza kuzuia malipo kwa kampuni hiyo ya kitapeli.

Hata hivyo, Lipumba alisema Rais Kikwete ameshindwa kabisa kusimamia masuala mazito ya nchi na yaliyomo ndani ya chama chake CCM na hivyo kusababisha matatizo makubwa nchini, ikiwa ni pamoja na kuyumba kwa dola na mpasuko wa chama tawala.

"Rais anawajua waliohusika na kashfa ya Richmond, lakini anajifanya mwema kwa makundi yote ya wabunge wa CCM; wale wanaojiita vinara wa kupambana na ufisadi na hata hao wanaotuhumiwa, hivyo ameshindwa kuchukua nafasi yake kama mwenyekiti na kusema waachie wenyewe,” alisema Lipumba.

Alifafanua kwamba hayo ndiyo matunda ya kuwa na kiongozi dhaifu asiye na uwezo wa kusimamia mambo mazito yanayoisumbua nchi.

Profesa Lipumba aliongeza kwamba katika malumbano ya wabune wa CCM kuna wale wanaoona kwamba Lowassa alionewa katika kashfa ya Richmond na kuna wanaoona alihusika kikamilifu na kile alichovuna ilikuwa ni haki yake.

Kuhusu posho mbili, Profesa Lipumba alisema suala hilo ni tatizo la msingi na kwamba, anawashangaa wale wanaotetea posho mbili kwa kazi moja.

“Bunge ni chombo kinachotakiwa kudhibiti mianya ya rushwa na kusimamia uwajibikaji wa serikali. Sasa leo wabunge wanapoenda kukagua mashirika ya umma itakuaje walazimishe kulipwa posho?” alihoji Profesa Lipumba.

“Huwezi kudai posho kwa sababu umeenda kukagua shirika la serikali kama mbunge, kwa sababu hali hiyo inapunguza na kudidimiza thamani ya bunge katika kutekeleza kazi zake katika jamii.”

Lipumba alitaka uwajibikaji kwa wale wote watakaobanainika kula posho mara mbili.

Alimshangaa spika wa Bunge, Samuel Sitta kwa kusema suala la posho hizo ni haki ya wabunge kwa sababu ni kama takrima tu na si rushwa wala ufisadi.

Tags:

0 comments

Post a Comment